Uncategorized

ZAO LA MKONGE LATAZAMWA KUONGEZA UZALISHAJI, SERIKALI YASUKUMA MAPINDUZI YA THAMANI

Written by Alex Sonna

Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

Serikali kupitia Bodi ya Mkonge Tanzania imeweka mkakati kabambe wa kuongeza uzalishaji wa zao la mkonge nchini kutoka tani 64,321.77 zilizofikiwa mwaka 2025/2026 hadi tani 80,000 katika mwaka wa kilimo 2026/2027, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha sekta hiyo muhimu kiuchumi.

Hayo yamesemwa leo Aprili 28, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Amesema Katika kufanikisha lengo hilo, Bodi imepanga kusambaza miche ya mkonge milioni 3.5 kwa wakulima ili kuongeza maeneo ya uzalishaji na kuboresha tija mashambani.

Aidha, kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Serikali itatoa mafunzo kwa wadau 200 na Maafisa Ugani 50 kuhusu mbinu bora za uzalishaji na uongezaji thamani wa zao la mkonge, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na ubora wa zao hilo sokoni.

Katika kuongeza thamani ya mkonge, Bodi itaendelea na ununuzi na usimikaji wa mashine 10 za kuchakata mkonge (dikotiketa) zenye uwezo wa kuchakata tani mbili kwa siku. Mashine hizo zitasimikwa katika mikoa ya Tanga, Morogoro, Shinyanga na Tabora, ili kurahisisha uchakataji wa zao hilo karibu na maeneo ya uzalishaji.

Vilevile, Serikali inakamilisha ujenzi wa vituo viwili vya kuchakata mkonge katika Wilaya za Mkinga na Handeni, hatua itakayosaidia kuongeza thamani ya zao hilo na kupunguza upotevu baada ya kuvunwa.

Katika kuimarisha masoko, Bodi ya Mkonge itaanzisha vituo 13 vya ukusanyaji na uuzaji wa mkonge kwa wakulima wadogo, sambamba na kuweka miundombinu ya uongezaji thamani kupitia mfumo wa brushing na baling katika mikoa ya Tanga, Pwani na Singida.

Hatua hizo zinalenga kuhakikisha wakulima wanapata masoko ya uhakika na bei nzuri ya mazao yao, huku pia zikichochea ushindani katika soko la mkonge ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wa miundombinu ya viwanda, Serikali inakamilisha ujenzi wa ghala, ofisi na mifumo ya maji taka katika viwanda vya Taula na Kibaranga vilivyopo Handeni na Muheza, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya uzalishaji.

Aidha, malipo ya mashine saba za kuchakata mkonge zinazomilikiwa na Kampuni ya Sisalana katika mashamba ya Hale, Magoma, Magunga, Ngombezi na Mwelya yamewekwa kipaumbele ili kuhakikisha zinaanza kufanya kazi kikamilifu.

Kwa ujumla, mikakati hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kuifanya sekta ya mkonge kuwa moja ya injini muhimu za uchumi kupitia ongezeko la uzalishaji, uongezaji thamani na upatikanaji wa masoko ya uhakika kwa wakulima.

About the author

Alex Sonna