Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.

Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.

Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali kupitia Wizara ya Kilimo na Bodi ya Pamba Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha uzalishaji wa zao la pamba nchini, huku ikiweka mikakati kabambe ya kuongeza thamani ya zao hilo na kuboresha maisha ya wakulima.
Hayo yamesemwa leo Aprili 28, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Lengo kuu la Serikali ni kufikia uzalishaji wa tani 400,000 za pamba ifikapo mwaka wa kilimo 2025/2026, sambamba na kusambaza pembejeo muhimu kwa wakulima, ikiwemo mbegu bora, viuatilifu na vifaa vya kisasa vya kilimo.
“Hadi kufikia Machi 2026, uzalishaji wa pamba umefikia tani 222,014 pekee, sawa na asilimia 55.5 ya lengo lililowekwa. Kupungua kwa uzalishaji kumeelezwa kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na mtawanyiko usioridhisha wa mvua katika maeneo mengi ya uzalishaji, hali iliyosababisha kudondoka kwa vitumba vya pamba.”amesema Mhe.Chongolo
Licha ya changamoto hiyo, Serikali imefanikiwa kusambaza pembejeo zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 61.8 kwa wakulima zaidi ya 510,000. Pembejeo hizo ni pamoja na tani 21,051 za mbegu bora, chupa zaidi ya milioni 9.5 za viuatilifu na vinyunyizi 80,000, hatua inayolenga kuongeza tija mashambani.
Katika kuendeleza kilimo hai, Bodi ya Pamba pia imesambaza lita 408,000 za mbolea hai, zitakazotumika katika zaidi ya hekta 10,000 za mashamba ya pamba.
Aidha, Serikali imenunua mashine 16 za kisasa za kupulizia viuatilifu, hatua itakayosaidia kupunguza adha kwa wakulima waliokuwa wakitumia vinyunyizi vya kubeba mgongoni, pamoja na kuongeza ufanisi katika udhibiti wa wadudu waharibifu.
Katika kuimarisha huduma za ugani, jumla ya Maafisa Ugani 761 wameajiriwa kupitia programu ya BBT kwa kushirikiana na sekta binafsi, lengo likiwa ni kuwafikia wakulima wengi zaidi kwa elimu na ushauri wa kitaalamu.
Mbali na uzalishaji, Serikali pia imejikita katika kuongeza thamani ya zao la pamba kupitia uwekezaji katika viwanda. Tayari maandalizi yanaendelea kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha kuchakata pamba kwa matumizi ya hospitali na kutengeneza nyuzi za kufungia tumbaku katika Halmashauri ya Itilima.
Vilevile, hatua zimefikiwa katika upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya kuanzisha kongani ya viwanda vya pamba katika Mkoa wa Simiyu, ambapo zaidi ya ekari 340 zinatarajiwa kutumika, huku wananchi wakipatiwa fidia stahiki.
Katika juhudi za kufufua miundombinu ya usindikaji, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeanza taratibu za kufufua viwanda vya kuchambua pamba (ginneries) katika maeneo ya Mhunze na Uzogole. Hatua hiyo inalenga kuwahakikishia wakulima soko la uhakika na kuongeza thamani ya mazao yao.
Kwa upande mwingine, jitihada za kuwawezesha vijana na wanawake zimeendelea, ambapo mashine za kusokota nyuzi na kutengeneza bidhaa za pamba kama vile vikoi na mitandio zimesambazwa katika baadhi ya maeneo, hatua inayochochea ajira na ujasiriamali.
Kwa ujumla, pamoja na changamoto ya hali ya hewa, juhudi za Serikali zinaonesha dhamira ya dhati ya kufufua na kuimarisha zao la pamba nchini, likiwa ni moja ya mazao muhimu ya biashara na chanzo kikubwa cha ajira na kipato kwa wananchi.