Featured Kitaifa

SERIKALI YAONGEZA NGUVU KILIMO HIMILIVU KUKABILIANA NA MABADILIKO YA TABIANCHI

Written by Alex Sonna

Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

Serikali imeongeza juhudi katika kuimarisha matumizi ya teknolojia na mbinu za kilimo kinachohimili mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni mkakati wa kulinda uzalishaji wa mazao na kuwasaidia wakulima kukabiliana na athari za hali ya hewa, hususan katika maeneo ya nyanda kame.

Hayo yamesemwa leo Aprili 28, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Amesema Kupitia Wizara ya Kilimo na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwemo kuimarisha uwezo wa Kituo cha TARI-Hombolo ili kuwa kitovu mahiri cha tafiti za mazao ya nyanda kame na teknolojia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

“Serikali imefanikiwa kugundua na kusambaza mbegu himilivu aina 54 za mazao mbalimbali ikiwemo choroko, maharage, mpunga, karanga, mtama na muhogo. Mbegu hizo zinalenga kuongeza uzalishaji na ustahimilivu wa mazao katika mazingira yenye changamoto za ukame na mvua zisizotabirika.”amesema 

Aidha, kituo cha TARI-Hombolo kimeboreshwa kwa kujengwa miundombinu ya kisasa ikiwemo kitalu nyumba (screen house) na mifumo ya umwagiliaji, hatua inayowezesha tafiti za kisasa na uzalishaji wa miche bora kwa wakulima.

Katika kuendeleza zao la tende, mashamba darasa manne yameanzishwa, huku miche 1,166 ikisambazwa kwa wakulima katika maeneo mbalimbali ya Dodoma na Pwani. Hatua hiyo inalenga kuhamasisha kilimo cha mazao yanayohimili ukame na kuongeza kipato kwa wakulima.

Sambamba na juhudi hizo, Serikali imeendelea kuandaa na kutekeleza mipango ya usimamizi wa mazingira katika sekta ya kilimo, ikiwa ni pamoja na mpango wa pili wa usimamizi wa mazingira unaolenga kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayosisitiza kilimo endelevu kinachozingatia uhifadhi wa mazingira.

Katika kuhakikisha miradi ya kilimo inazingatia viwango vya mazingira, tathmini za athari za mazingira na jamii zimeendelea kufanyika katika miradi 24, huku hatua za kudhibiti athari hizo zikichukuliwa ili kulinda mazingira na jamii zinazozunguka miradi hiyo.

Kwa upande wa elimu, Wizara imefanikiwa kutoa mafunzo kwa zaidi ya wanufaika 23,000 wakiwemo wakulima, maafisa ugani, watafiti na wadau wengine wa sekta ya kilimo kuhusu mbinu za kilimo himilivu, uhifadhi wa mazingira na matumizi sahihi ya teknolojia za kisasa.

Mafunzo hayo yametolewa katika mikoa mbalimbali nchini ikiwemo Arusha, Dodoma, Morogoro, Mwanza, Tanga na Tabora, yakilenga kuongeza uelewa na uwezo wa wadau katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

About the author

Alex Sonna