Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeweka mikakati kabambe ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta nchini ili kupunguza utegemezi wa mafuta ya kula kutoka nje ya nchi, hali inayoiweka nchi kutumia fedha nyingi za kigeni kufidia upungufu wa bidhaa hiyo muhimu.
Hayo yamesemwa leo Aprili 28, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Amesema mahitaji ya mafuta ya kula nchini ni takriban tani 731,974 kwa mwaka, wakati uzalishaji wa ndani ni tani 305,906 pekee, hivyo kuacha pengo kubwa la tani 426,068 ambalo hulazimu uagizaji kutoka nje.
“Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Wizara ya Kilimo imepanga kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta kutoka tani 2,248,046.24 mwaka 2024/2025 hadi tani 2,300,000 katika mwaka 2026/2027 kupitia mafunzo ya kilimo bora kwa wakulima katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji.”amesema
Aidha, Serikali itaweka msukumo katika kilimo cha kibiashara kwa kuanzisha mashamba makubwa ya pamoja yenye ukubwa wa hekta 48,000 kwa ajili ya zao la chikichi na alizeti katika mikoa ya Kigoma, Morogoro, Singida na Dodoma.
Katika kuongeza uzalishaji wa mbegu na miche, Wizara itasambaza mbegu bora za alizeti tani 120 kwa wakulima kupitia mpango wa ruzuku, pamoja na kuzalisha na kusambaza miche milioni 2 ya chikichi katika maeneo ya uzalishaji.
Vilevile, Serikali itaratibu upatikanaji na usambazaji wa mbegu bora za karanga tani 20.1 pamoja na mbegu za ufuta tani 100, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta nchini.
Aidha, Wizara inakamilisha Mkakati wa Kitaifa wa Mafuta ya Kula (National Edible Oil Strategy), utakaolenga kuongeza uzalishaji wa ndani na hatimaye kuifikisha nchi katika kujitosheleza kwa mafuta ya kula.
Kwa ujumla, hatua hizi zinatarajiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa uagizaji wa mafuta kutoka nje, kuimarisha usalama wa chakula, kuongeza ajira na kukuza uchumi wa wakulima nchini.