Featured Kitaifa

ZAO LA MKONGE LAPATA MSUKUMO MPYA, UZALISHAJI WAFIKIA ASILIMIA 80 YA LENGO

Written by Alex Sonna

Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 28,2026 bungeni Dodoma.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

Serikali kupitia Wizara ya Kilimo na Bodi ya Mkonge Tanzania imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kufufua na kuimarisha zao la mkonge nchini, baada ya uzalishaji wake kufikia tani 64,321.77 hadi Machi 2026, sawa na asilimia 80.4 ya lengo la tani 80,000 kwa mwaka wa kilimo 2025/2026.

Hatua hiyo inatajwa kuwa ishara ya mafanikio ya jitihada zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kukuza zao hilo la kimkakati, linalochangia ajira na mapato kwa maelfu ya Watanzania.

Hayo yamesemwa leo Aprili 28, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Katika kufanikisha hilo, Serikali imewekeza katika utoaji wa mafunzo kwa wadau wa zao la mkonge, ambapo jumla ya wakulima na wadau 6,853 pamoja na Maafisa Ugani 44 wamepatiwa elimu ya uzalishaji bora na uongezaji thamani katika mikoa mbalimbali ikiwemo Tanga, Morogoro, Pwani, Simiyu na Kilimanjaro.

Sambamba na hilo, mashamba makubwa ya pamoja ya wakulima wadogo yameanzishwa na kufikia ukubwa wa hekta 9,211 katika mikoa ya Tanga, Morogoro, Pwani na Kilimanjaro. Hatua hiyo inalenga kuongeza tija na kuimarisha uzalishaji wa mkonge kwa kutumia mbinu za kisasa na usimamizi wa pamoja.

Katika kuhakikisha upatikanaji wa ardhi ya kilimo, Serikali imewezesha umiliki wa zaidi ya hekta 21,625 katika mikoa ya Tanga, Morogoro na Arusha, jambo linalotarajiwa kuongeza uzalishaji wa mkonge kufikia tani 120,000 ifikapo mwaka 2030.

Katika kuongeza thamani ya zao hilo, Bodi ya Mkonge imeanzisha kiwanda cha kuchakata mkonge chenye uwezo wa kuchakata tani tano kwa siku katika Mkoa wa Tanga. Aidha, maandalizi ya ujenzi wa viwanda vingine viwili katika Wilaya za Handeni na Mkinga yanaendelea baada ya kupatikana kwa mzabuni.

Hatua nyingine muhimu ni kuanzishwa kwa Chama Kikuu cha Ushirika wa Mkonge Mkoa wa Tanga (Tanga Sisal Cooperative Union Ltd), kitakachoratibu shughuli za vyama vya msingi na kusaidia wakulima kupata masoko na huduma muhimu.

Katika ubunifu wa matumizi ya mabaki ya mkonge, Serikali inaendelea na ujenzi wa kituo cha kuzalisha nzi chuma (Black Soldier Flies) kitakachotumia mabaki ya mkonge kuzalisha protini kwa ajili ya chakula cha mifugo, hatua inayolenga kuongeza thamani na kupunguza upotevu wa rasilimali.

Aidha, jitihada za kurejesha viwanda na mashamba yaliyokuwa chini ya Kampuni ya Sisalana zinaendelea, lengo likiwa ni kuongeza uzalishaji na kuimarisha sekta ya uchakataji wa mkonge nchini.

About the author

Alex Sonna