Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA) imeendelea kuimarisha mfumo wa usimamizi wa vipimo nchini kwa kuboresha mazingira ya utendaji kazi, kununua vifaa vya kisasa vya ukaguzi pamoja na kuongeza mapambano dhidi ya biashara haramu ya mazao maarufu kama “Lumbesa.”
Hatua hiyo inalenga kulinda haki za wakulima, wafanyabiashara na watumiaji kwa kuhakikisha biashara zote zinafanyika kwa kutumia vipimo sahihi vinavyokubalika kisheria.
Hayo yamesemwa leo Mei 22, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Ofisi Mpya Kujengwa Lindi na Songwe
Katika kuimarisha huduma zake nchini, Wizara imeanza mchakato wa ujenzi wa ofisi mpya za Wakala wa Vipimo katika mikoa ya Lindi na Songwe.
Amesema kuwa hadi Aprili 2026, hatua ya usanifu na michoro ya majengo hayo imekamilika na kinachosubiriwa sasa ni kutangazwa kwa zabuni ili kumpata mkandarasi wa ujenzi.
Wataalamu wanaeleza kuwa ujenzi wa ofisi hizo utarahisisha utoaji wa huduma za uhakiki wa vipimo kwa wananchi na wafanyabiashara katika maeneo hayo ambayo yamekuwa yakikua kwa kasi kiuchumi.
Vifaa vya Kisasa Vyaboresha Ufanisi
Sambamba na hilo, Wakala wa Vipimo umefanya maboresho makubwa ya kiteknolojia kwa kununua vifaa mbalimbali vya kisasa vya TEHAMA na vifaa vya kitaalam vitakavyoongeza uwezo wa ukaguzi wa vipimo nchini.
Miongoni mwa vifaa vilivyonunuliwa ni pamoja na laptop 35, desktop 28, scanner mbili, printer 20 za multifunction pamoja na mashine za kisasa za kupimia na kuhakiki uzito na ujazo.
Vifaa vingine vya kitaalam vilivyonunuliwa ni pamoja na Digital Thermometer, Electronic Balances, Flow Meters, Proving Tanks pamoja na vifaa maalum vya ukaguzi wa mizani na pampu za gesi.
Kwa mujibu wa Wizara, upatikanaji wa vifaa hivyo utaongeza wigo wa huduma katika maeneo mapya na kurahisisha uhakiki wa vipimo kwa wananchi karibu na maeneo yao.
Serikali Yakaza Kamba Dhidi ya “Lumbesa”
Serikali imeendelea na mapambano dhidi ya vitendo vya ufungashaji na usafirishaji wa mazao kinyume cha sheria maarufu kama “Lumbesa.”
Kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura ya 340, mazao yanayofungashwa kwa uzito hayapaswi kuzidi kilogramu 100 pamoja na kiwango cha ziada kinachoruhusiwa cha asilimia tano.
Sheria hiyo pia inawataka wafanyabiashara kutumia mizani iliyohakikiwa rasmi na Wakala wa Vipimo angalau mara moja kwa mwaka.
Hata hivyo, Serikali imebaini baadhi ya wafanyabiashara kuendelea kukiuka sheria hiyo kwa kufungasha mazao kupita kiwango kinachoruhusiwa jambo linalosababisha hasara kwa wakulima, wasafirishaji na wanunuzi.
Magari 81 Yakutwa na Makosa
Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Wizara kupitia Wakala wa Vipimo imeendesha operesheni maalum katika mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Tanga, Pwani, Morogoro, Mbeya, Iringa na Njombe.
Kupitia operesheni hizo, jumla ya magari 2,500 yaliyokuwa yakisafirisha mazao mbalimbali yalikaguliwa.
Kati ya hayo, magari 2,419 yalibainika kufuata sheria kwa kusafirisha mazao yaliyofungashwa kwa uzito unaoruhusiwa, huku magari 81 yakikutwa yakiwa na makosa ya kuzidisha uzito wa vifurushi.
Hatua kali zilichukuliwa dhidi ya wahusika ikiwemo kutozwa faini za papo kwa papo na kuamriwa kufungasha upya mazao yao kwa kufuata sheria.
Huduma Zasogezwa Karibu na Wananchi
Katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa urahisi zaidi, Serikali imeanzisha vituo vya muda 5,050 vya uhakiki wa vipimo katika maeneo ya kata, vijiji na mitaa nchi nzima.
Aidha, baadhi ya halmashauri zikiwemo Mpanda, Kasulu na Kibondo zimeanza kutunga sheria ndogo zinazosisitiza matumizi ya mizani iliyohakikiwa katika biashara ya mazao.
Jitihada hizo zinaonyesha dhamira ya Serikali ya kujenga mfumo wa biashara wenye usawa, unaozingatia sheria na unaolinda haki za kila mshiriki wa uchumi.