Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 30,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Uwekezaji Waongezeka, Ajira Zaongezeka, Uchumi Waimarika
Tanzania imeendelea kuandika historia mpya katika sekta ya viwanda na biashara huku Serikali ikiendeleza juhudi za kujenga uchumi wa kisasa unaotegemea uzalishaji wa ndani, kuongeza thamani ya malighafi na kukuza ajira kwa wananchi. Katika mwaka wa fedha 2025/2026, mafanikio makubwa yameendelea kushuhudiwa ambapo viwanda vipya vikubwa na vya kati 25 vimejengwa na kuanza uzalishaji katika maeneo mbalimbali nchini.
Hayo yamesemwa leo Mei 22, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Amesema ukuaji huo wa sekta ya viwanda umechochea upatikanaji wa ajira 39,250, zikiwemo ajira za moja kwa moja 7,635 na zisizo za moja kwa moja 31,615. Serikali inaeleza kuwa mafanikio hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 inayolenga kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati unaotegemea viwanda.
Viwanda vya Mabati Vyapanua Soko la Kikanda
Sekta ya uzalishaji wa mabati imeendelea kufanya vizuri ambapo Tanzania sasa ina viwanda vitano vikubwa vya mabati vyenye uwezo wa kuzalisha tani 410,000 za mabati ya rangi na tani 700,000 za mabati meupe kwa mwaka. Viwanda hivyo ni Lodhia, MMI Steel, ALAF Limited, Kinglion pamoja na GSM Roofing Sheet.
Hadi Aprili 2026, viwanda hivyo vilikuwa vimezalisha tani 350,000 za mabati ya rangi na tani 500,000 za mabati meupe, kiwango kinachokidhi mahitaji ya ndani na kuruhusu ziada kuuzwa katika nchi jirani kama Burundi, Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Malawi.
Kiwanda kipya cha GSM Roofing Sheet kilichopo Dar es Salaam kimeonekana kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati, kikiajiri watu zaidi ya 3,800 moja kwa moja na kwa njia zisizo za moja kwa moja.
Amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) inaendelea na utekelezaji wa mradi mkubwa wa Maganga Matitu kwa kushirikiana na kampuni ya Fijuan Hexingwang Industry Tanzania Co. Ltd, hatua inayotarajiwa kupunguza utegemezi wa malighafi za chuma kutoka nje ya nchi.
Uzalishaji wa Saruji Wazidi Mahitaji ya Ndani
Katika sekta ya saruji, Tanzania sasa ina viwanda 15 vyenye uwezo wa kuzalisha tani milioni 13.6 kwa mwaka. Hadi Aprili 2026, uzalishaji ulikuwa umefikia tani milioni 10.3 huku mahitaji ya ndani yakiwa tani milioni 8.5 pekee.
Hii inaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa saruji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Saruji ya ziada imeendelea kuuzwa katika masoko ya Malawi, Zambia, Rwanda, Burundi na DRC.
Kiwanda kipya cha WIH Holding Limited kilichopo Kigoma nacho kimeongeza nguvu katika uzalishaji huo baada ya kuanza kuzalisha tani milioni 1.5 za saruji ndani ya kipindi kifupi tangu kuanza shughuli zake.
Sukari
Katika hatua ya kupunguza uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi, Serikali imeendelea kuimarisha viwanda vya ndani kupitia upanuzi wa miradi mbalimbali.
Kwa sasa Tanzania ina viwanda saba vya sukari vyenye uwezo wa kuzalisha tani 800,000 kwa mwaka. Hadi Aprili 2026 uzalishaji ulikuwa umefikia tani 410,979 huku mahitaji ya taifa yakiwa tani 550,000.
Upanuzi mkubwa umefanywa katika viwanda vya Kilombero Sugar Company Limited na Mkulazi Holding Company Limited. Kiwanda cha Kilombero kinatarajiwa kuongeza uzalishaji kutoka tani 123,000 hadi tani 226,000 kwa mwaka kuanzia Juni 2026.
Aidha, Mkulazi imeanza uzalishaji wa sukari ya viwandani (industrial sugar), hatua itakayosaidia sekta nyingine za uzalishaji zinazotegemea sukari kama malighafi.
Viwanda vya Dawa Vyaleta Tumaini Sekta ya Afya
Sekta ya afya nayo imeendelea kunufaika na uwekezaji mkubwa wa viwanda vya dawa na vifaa tiba. Katika mwaka 2025/2026, jumla ya viwanda 11 vipya vya dawa na vifaa tiba vimejengwa na kuanza majaribio ya uzalishaji.
Viwanda hivyo vina uwezo wa kuzalisha vizio bilioni 3.5 vya dawa za binadamu huku vikitoa ajira zaidi ya 25,000.
Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mkakati wa Serikali wa kupunguza utegemezi wa dawa kutoka nje ya nchi na kufikia uwezo wa kuzalisha asilimia 60 ya mahitaji ya dawa nchini ifikapo mwaka 2035.
Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industries (TPI) cha Arusha nacho kinaendelea kufanyiwa ukarabati kwa ajili ya kuanza uzalishaji wa dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI (ARV).
Mafuta ya Kula: Serikali Yaongeza Mapambano ya Kujitegemea
Pamoja na Tanzania kuwa na viwanda zaidi ya 1,600 vya mafuta ya kula, uzalishaji wa ndani bado haujakidhi mahitaji ya taifa. Kwa sasa uzalishaji ni tani 302,000 pekee dhidi ya mahitaji ya tani 700,000 kwa mwaka.
Kutokana na hali hiyo, Serikali imeongeza juhudi za kuhamasisha uzalishaji wa mbegu bora za alizeti, utoaji wa ruzuku ya mbolea na uwekezaji katika teknolojia za uchakataji.
Miongoni mwa viwanda vipya vilivyoanza kazi ni Vion Win Ltd cha Singida pamoja na Mainland Group Agro Process Co. Ltd cha Dodoma ambacho kimeongeza uwezo wa kusindika alizeti kutoka tani 75,000 hadi tani 150,000 kwa mwaka.
Viwanda Vipya Vyafungua Fursa Mpya
Mbali na sekta hizo kubwa, viwanda vingine vipya pia vimeendelea kujengwa nchini. Baadhi yake ni Afriport Apparel cha Dar es Salaam kinachozalisha mavazi maalum ya kujikinga kazini, Giant Group Co. Ltd cha Pwani kinachotengeneza nyaya na vifaa vya umeme, pamoja na FarmBase cha Kigamboni kinachozalisha dawa za mifugo na virutubisho.