Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Waziri wa Viwanda na Biashara Judithi Kapinga amevitaja vipaumbele saba vya kimkakati kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza uchumi wa viwanda, kuongeza ajira, kuimarisha biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya Nchi.
Kapinga amevitaja vipaumbele hivyo wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hiyo Bungeni Jijini Dodoma kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ambapo amesema serikali itaendelea kuwezesha uanzishwaji na uendelezaji wa viwanda nchini ili kuongeza thamani ya mazao.
Waziri Kapinga amesema utekelezaji wa vipaumbele hivyo unalenga kuongeza ajira kwa wananchi, kuongeza mapato ya serikali, kukuza uchumi wa Taifa na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji wa viwandani na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.
Kapinga amesema wizara itaendelea kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani kwa kuboresha mazingira wezeshi ya uwekezaji pamoja na kuendeleza miundombinu ya maeneo ya viwanda na kongani za viwanda kwa ajili ya viwanda vidogo, vya kati na vikubwa.
Aidha,amesema serikali itaendelea kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara kwa kupunguza vikwazo visivyo vya kikodi, kurahisisha taratibu za biashara na kuchochea ukuaji wa sekta binafsi ili kuongeza ushindani.