Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali kupitia Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kinaendelea kuimarika na kuwa kitovu muhimu cha elimu ya biashara na teknolojia nchini kufuatia uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia.
Katika hatua nyingine kubwa ya maendeleo ya elimu ya juu, Wizara kupitia CBE inaendelea na ujenzi wa jengo la kisasa la ghorofa 10 lijulikanalo kama Metrology Complex katika kampasi ya Dar es Salaam, mradi unaotarajiwa kubadilisha kabisa mazingira ya utoaji wa elimu chuoni hapo.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026-2027,bungeni Waziri wa Viwanda na Biashara,Judith Kapinga,amesema hadi Aprili 2026 ujenzi wa jengo hilo ulikuwa umefikia asilimia 93 ambapo zaidi ya shilingi bilioni 8.88 tayari zimetumika kati ya shilingi bilioni 10.39 zilizotengwa kwa hatua ya kwanza ya mradi huo.
Jengo hilo litakapokamilika litakuwa na jumla ya kumbi 29 za mihadhara zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 4,160 kwa wakati mmoja, hatua inayotarajiwa kupunguza changamoto ya uhaba wa maeneo ya kujifunzia na kuongeza ubora wa elimu.
Sambamba na ujenzi wa miundombinu, CBE imeendelea kufanya maboresho makubwa ya mitaala ili kuendana na kasi ya maendeleo ya teknolojia na mahitaji ya soko la ajira.
Waziri Kapinga ameeleza kuwa chuo hicho sasa kinaweka mkazo mkubwa katika elimu ya vitendo kupitia Programu ya Uanagenzi ambayo itawawezesha wanafunzi kutumia sehemu ya muda wao darasani na sehemu nyingine katika maeneo ya kazi ili kupata uzoefu wa moja kwa moja.
Mpango huo unaelezwa kuwa ni hatua muhimu ya kuwaandaa wahitimu wenye ujuzi unaohitajika katika dunia ya sasa ya biashara na teknolojia.
Hadi Aprili 2026, mitaala mipya minane ilikuwa tayari imeidhinishwa na kufanya jumla ya mitaala iliyopitishwa kufikia 71, huku mitaala mingine 28 ikiwa katika hatua mbalimbali za maandalizi na uhakiki.
Amesema maboresho hayo ya miundombinu na mitaala yameendelea kuongeza mvuto wa chuo hicho kwa wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Takwimu zinaonyesha kuwa udahili wa wanafunzi umeongezeka kutoka wanafunzi 20,029 katika mwaka wa masomo 2023/2024 hadi wanafunzi 24,957 mwaka 2025/2026, sawa na ongezeko la wanafunzi 4,928 ndani ya kipindi kifupi.
Ongezeko hilo linaonyesha kuongezeka kwa mahitaji ya elimu ya biashara na taaluma zinazohusiana na uchumi wa kisasa unaotegemea maarifa na teknolojia.
Kupitia miradi hiyo, Serikali inalenga kuhakikisha taasisi za elimu ya juu zinaendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia pamoja na mahitaji ya uchumi wa viwanda na biashara.