Kaimu Mtendaji Mkuu wa UCSAF,Mhandisi Albert Richard wakati akitoa wasilisho katika mafunzo ya wahariri wa vyombo vya habari Mkoa wa Dodoma yaliyofanyika Mei 15, 2026.
Na .Alex Sonna,Mzalendo blog -DODOMA
Katika hatua nyingine ya kuimarisha uchumi wa kidijitali nchini, Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umeendelea kutekeleza mradi mkubwa wa kuongeza uwezo wa minara ya mawasiliano kutoka teknolojia ya 2G kwenda 3G na 4G, hatua inayotarajiwa kuleta mapinduzi makubwa ya huduma za intaneti vijijini.
Hayo yameelezwa na Kaimu Mtendaji Mkuu wa UCSAF,Mhandisi Albert Richard wakati akitoa wasilisho katika mafunzo ya wahariri na waandishi wa habari kutoka vyombo vya habari Mkoa wa Dodoma yaliyofanyika Mei 15, 2026.
Amesema Mradi huo unahusisha uboreshaji wa minara 62 ya mawasiliano katika maeneo mbalimbali yasiyo na mvuto wa kibiashara, ukiwa na lengo la kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma bora za mawasiliano na intaneti yenye kasi kama ilivyo katika maeneo ya mijini.
” Kampuni ya Vodacom tayari imekamilisha utekelezaji wa minara 37, ambayo sasa inaendelea kutoa huduma za intaneti yenye kasi kwa wananchi wa maeneo husika. Hatua hiyo imeanza kufungua fursa mpya za kiuchumi na kijamii kwa wakazi wa vijijini waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya mtandao hafifu kwa muda mrefu.”amesema Mhandisi Richard
Aidha, minara mingine 25 inayotekelezwa na Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), ipo katika hatua za awali za manunuzi, huku Serikali ikieleza dhamira yake ya kuhakikisha utekelezaji wa mradi huo unakamilika kwa wakati ili kuongeza usawa wa kidijitali nchini.
Hata hivyo amesema kuwa uboreshaji wa minara hiyo unatajwa kuwa hatua muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kidijitali, ambapo wananchi wataweza kutumia kwa urahisi huduma mbalimbali zinazotegemea intaneti ikiwemo elimu mtandao, afya mtandao, biashara mtandao na huduma za kifedha kupitia simu za mkononi.
Wataalamu wa sekta ya mawasiliano wanaeleza kuwa kuboreshwa kwa teknolojia kutoka 2G kwenda 3G na 4G kutasaidia kuongeza kasi ya intaneti, ubora wa mawasiliano na upatikanaji wa huduma za kidijitali katika maeneo ya vijijini ambayo kwa miaka mingi yamekuwa nyuma kiteknolojia.
Mbali na kuboresha mawasiliano, mradi huo pia unatarajiwa kuchochea shughuli za kiuchumi kwa kuwawezesha wananchi kutumia mifumo ya malipo ya kidijitali, kufanya biashara mtandaoni, kupata taarifa za masoko kwa haraka pamoja na kuongeza ajira kupitia matumizi ya teknolojia.
Katika sekta ya elimu, wanafunzi na walimu vijijini wataweza kupata rasilimali za kujifunzia mtandaoni kwa urahisi zaidi, huku sekta ya afya nayo ikinufaika kupitia huduma za ushauri na tiba kwa njia ya mtandao.
UCSAF imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia Watanzania wote bila kujali mazingira ya kijiografia au mvuto wa kibiashara wa eneo husika.
Kupitia miradi hiyo, Serikali inaendelea kutimiza azma ya kujenga Tanzania ya kidijitali yenye wananchi wanaounganishwa na teknolojia, taarifa na fursa za maendeleo kwa usawa.