Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote nchini (UCSAF), imeendelea kuimarisha sekta ya mawasiliano kwa kuanza utekelezaji wa Mradi wa Kufikisha Mawasiliano Vijijini Awamu ya Kumi (10), utakaohusisha ujenzi wa minara 287 ya mawasiliano katika kata 287 nchini.
Hayo yameelezwa jijini Dodoma na Kaimu Mkurugenzi wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), ,Mhandisi Albert Richard,wakati wa semina ya wahariri na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vilivyoandaliwa na mfuko huo
Amesema uzinduzi rasmi wa kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo ulifanyika tarehe 5 Desemba 2025, ambapo utekelezaji wake unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 15 kwa gharama ya zaidi ya Shilingi bilioni 29 zilizotengwa na Serikali.
Mradi huo mkubwa unalenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika maeneo ya vijijini ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakikabiliwa na changamoto ya mtandao hafifu au kutokuwa kabisa na huduma za simu na intaneti.
“Jumla ya wakazi zaidi ya milioni 2.9 watanufaika moja kwa moja na utekelezaji wa mradi huo katika mikoa 29 ya Tanzania Bara na Zanzibar.”amesema Mhandisi Richard
Miongoni mwa mikoa itakayopata minara mingi zaidi ni Mwanza yenye minara 24 katika vijiji 30, ikifuatiwa na Manyara yenye minara 16 katika vijiji 20, pamoja na Mkoa wa Mbeya ambao utapata minara 16 katika vijiji 28.
Mikoa mingine yenye idadi kubwa ya wanufaika ni pamoja na Rukwa yenye wakazi zaidi ya 250,000 watanufaika, Manyara wakazi zaidi ya 199,000, Simiyu zaidi ya 179,000 pamoja na Singida yenye zaidi ya wakazi 174,000 watakaofikiwa na huduma hizo muhimu.
Aidha, mradi huo unatarajiwa kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa maeneo ya vijijini kupitia urahisi wa kupata taarifa, huduma za kifedha kidijitali, elimu kwa njia ya mtandao pamoja na huduma za afya mtandao.
Serikali imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za mawasiliano bila kujali eneo analoishi, hatua ambayo inaendana na ajenda ya taifa ya uchumi wa kidijitali na maendeleo jumuishi.
Kupitia mradi huo wa Awamu ya Kumi, Tanzania inaendelea kupiga hatua katika kupunguza pengo la kidijitali kati ya mijini na vijijini, huku wananchi wakitarajia kuona maboresho makubwa ya huduma za mawasiliano katika maeneo yao ndani ya kipindi kifupi kijacho.
