Featured Kitaifa

KUELEKEA KILELE CHA SIKU YA WANAWAKE DUNIAN, NSSF YAKABIDHI VIFAA VYA TIBA KITUO CHA AFYA MAHUTA

Written by mzalendoeditor
Katika kuelekea kuadhimisha siku ya wanawake duniani, ambayo huadhimishwa kila ifikapo tarehe 8 Machi, Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umetoa msaada wa vifaa vya tiba mbalimbali ambavyo vitatumiwa na akina mama wakati wa kujifungua katika kituo cha Afya Mahuta kilichopo Wilaya ya Tandahimba mkoani Mtwara.
 
Vifaa vya tiba hivyo vilikabidhiwa tarehe 4 Machi, 2024 na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa NSSF, Bi. Vaileth Segeja. Vifaa vya tiba vilivyokabidhiwa ni pamoja na vitanda vitatu vya kujifungulia wakina mama, seti tatu za kujifungulia ‘delivery kit’, mashine moja ya kusaidia kupumua, mayo table mbili, mashine tatu za kusikiliza mapigo ya moyo ya mtoto aliyezaliwa(neonatal stethoscope), kifaa maalum cha kutolea uchafu puani na mdomoni kwa mtoto aliyezaliwa na uchafu(penguin sucker) , mashine ya kusikiliza mapigo ya moyo ya mtoto akiwa tumboni (Fetal doppler), mizani miwili ya kidijitali ya kupima uzito watoto (digital neonatal weighing scales).
 
Akipokea vifaa vya tiba hivyo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tandahimba, ACI Mariam Mwanzalima, aliishukuru NSSF kwa kutoa msaada huu ambao unakwenda kuboresha zaidi huduma za afya katika kituo cha Mahuta hasa kwa mama na mtoto.
 
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mahuta, Dkt. Leopold Nkayamba aliishukuru NSSF kwa msaada huo kwani kituo hicho kilikuwa na uhitaji wa vifaa hivyo. Kituo cha Afya Mahuta kinahudumia wananchi 16,596 wakiwemo wanawake 8,860 na wanaume 7,736 na kinahudumia vijiji vinane, ambapo kwa mwezi wanaojifungua katika kituo hicho ni wastaani wa 75 – 100.

About the author

mzalendoeditor