Rais wa Jamhuri ya Kenya Dkt.William Ruto amesema mtihani wa kweli wa ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) upo katika uwezo wa nchi wanachama kukuza biashara, akisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kubadilika na kuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi.
Akilihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Dodoma leo Jumanne, Mei 5, 2026, Dkt.Ruto amesema licha ya mafanikio yaliyofikiwa, bado kuna nafasi kubwa ya kuongeza biashara ya ndani ya ukanda huo ili kuleta manufaa zaidi kwa wananchi wa Afrika Mashariki.
Amesema ushirikiano wa EAC haupaswi kubaki katika makubaliano ya kisiasa pekee, bali uonekane kwa vitendo kupitia ongezeko la uwekezaji, ajira na biashara kati ya nchi wanachama.
“Tunapaswa kuhakikisha kuwa EAC inakuwa nguvu halisi ya kiuchumi inayozalisha fursa na ustawi kwa wananchi wetu,” amesema Ruto, akisisitiza umuhimu wa kuondoa vikwazo vinavyozuia biashara kuvuka mipaka.
Rais huyo amebainisha kuwa takwimu zinaonesha ukuaji wa biashara ndani ya ukanda huo, lakini bado hazijafikia kiwango kinachotarajiwa. Akinukuu taarifa kutoka Sekretarieti ya EAC, amesema biashara ya jumla ya ukanda iliongezeka kutoka dola bilioni 124.9 mwaka 2024 hadi dola bilioni 156.6 mwaka 2025, sawa na ongezeko la zaidi ya asilimia 25.
Aidha, biashara ya ndani ya EAC iliongezeka kwa asilimia 28, kutoka dola bilioni 15.1 hadi dola bilioni 19.3, hatua inayoashiria mwelekeo mzuri wa ushirikiano wa kiuchumi, ingawa bado ni sehemu ndogo ya biashara yote ya ukanda.
Ruto amesema takwimu hizo zinaonesha mafanikio yanayoanza kuonekana, lakini pia zinaweka wazi kazi kubwa iliyobaki katika kuhakikisha soko la pamoja la Afrika Mashariki linatumika kikamilifu.
Amesisitiza kuwa nchi wanachama zinapaswa kuongeza juhudi katika kuimarisha miundombinu, kurahisisha sera za biashara na kuondoa vikwazo visivyo vya lazima ili kuchochea ukuaji wa biashara ya ndani ya ukanda huo.