Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 22,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali kupitia Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni BRELA imeendelea kuimarisha utoaji wa elimu na huduma kwa wananchi kupitia kliniki za biashara zilizofanyika katika mikoa mbalimbali nchini, zikiwa sehemu ya juhudi za kusogeza huduma karibu na wananchi na kurahisisha urasimishaji wa biashara.
Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026-2027,bungeni Waziri wa Viwanda na Biashara,Judith Kapinga,amesema kuwa kliniki hizo zimekuwa zikifanyika sambamba na matukio makubwa ya kitaifa na shughuli za taasisi mbalimbali, hatua iliyosaidia kufikia idadi kubwa ya wafanyabiashara na wananchi katika maeneo tofauti nchini.
Amesema kuwa miongoni mwa kliniki hizo ni ile iliyofanyika katika Mkoa wa Mwanza wakati wa michezo ya SHIMIWI, ambapo wafanyabiashara walipata nafasi ya kupata elimu kuhusu usajili wa biashara, utoaji wa leseni pamoja na huduma mbalimbali za BRELA.
Kliniki nyingine ilifanyika katika Mkoa wa Dar es Salaam wakati wa Wiki ya Huduma kwa Mteja, ambapo wananchi wengi walijitokeza kupata huduma moja kwa moja pamoja na kuuliza maswali kuhusu taratibu za kuanzisha na kuendesha biashara rasmi.
Aidha, kliniki nyingine muhimu ilifanyika katika Mkoa wa Morogoro wakati wa michezo ya SHIMMUTA, ambapo wafanyabiashara na wananchi walipata fursa ya kusajili biashara zao na kupata maelekezo ya moja kwa moja kutoka kwa wataalamu wa BRELA.
Kupitia kliniki hizo, wananchi wamepata fursa ya kupata huduma za karibu, kupunguza changamoto za kiutendaji na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa biashara zilizosajiliwa rasmi katika kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.
Serikali imeeleza kuwa mpango huo utaendelea kuimarishwa ili kuhakikisha huduma za usajili na elimu ya biashara zinawafikia wananchi wengi zaidi, hususan katika maeneo ya pembezoni na makundi ya wafanyabiashara wadogo na wa kati.