Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 15, 2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeeleza dhamira yake ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha utalii wa mikutano na matukio ya kimataifa barani Afrika kupitia mikakati mipya ya kukuza Sekta ya Utalii, hatua inayotarajiwa kuongeza mapato ya Taifa, ajira na idadi ya watalii wanaoingia nchini.
Hayo yamesemwa leo Mei 15, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Dkt.Kijaji amesema kuwa mkakati huo umetajwa kuwa sehemu ya utekelezaji wa Ibara ya 23 ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030 inayotambua Sekta ya Utalii kama injini muhimu ya maendeleo ya uchumi na jamii.
Aidha amesema kuwa lengo kuu ni kuongeza mchango wa Sekta ya Utalii katika Pato la Taifa kutoka asilimia 17 mwaka 2025 hadi kufikia asilimia 20 ifikapo mwaka 2030 kupitia matumizi ya mbinu za kisasa za utangazaji pamoja na kuimarisha utalii wa mikutano, maonesho na matukio maalum maarufu kama MICE (Meetings, Incentives, Conferences and Exhibitions).
Waziri Kijaji amesema Serikali imeanza kutumia matukio makubwa ya kimataifa kama jukwaa la kuitangaza Tanzania duniani, sambamba na kuvutia wawekezaji na watalii kutoka mataifa mbalimbali.
“Utalii wa mikutano na matukio ni fursa kubwa kwa uchumi wetu. Wageni wanaokuja kushiriki mikutano au maonesho huongeza matumizi kwenye hoteli, usafiri, huduma za chakula na biashara nyingine nyingi,” amesema Waziri Kijaji
Katika miaka ya hivi karibuni, Tanzania imeendelea kupata mafanikio makubwa katika kuandaa mikutano na matukio ya kimataifa kutokana na kuimarika kwa miundombinu ya usafiri, viwanja vya ndege, huduma za hoteli pamoja na mazingira ya uwekezaji.
Wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa utalii wa MICE ni moja ya sekta zinazokua kwa kasi duniani kutokana na uwezo wake wa kuleta wageni wenye matumizi makubwa na kuongeza mzunguko wa fedha katika uchumi wa ndani.
Aidha, Serikali imeeleza kuwa itaendelea kupanua wigo wa mazao ya utalii kwa kuunganisha vivutio vya asili, utamaduni, michezo, burudani na matukio ya kimataifa ili kuifanya Tanzania kuwa kivutio kikubwa zaidi cha utalii Afrika Mashariki.
Mbali na kuongeza mapato ya Taifa, mkakati huo pia unatarajiwa kufungua maelfu ya ajira mpya kwa vijana katika sekta za huduma, usafirishaji, teknolojia, uandaaji wa matukio na biashara ndogo ndogo zinazohudumia watalii.
Serikali inaendelea kushirikiana na sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na ushindani wa soko la utalii duniani kupitia mikakati ya kisasa ya matangazo na uboreshaji wa huduma za utalii.