NAIBU Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Ndege Qwaray,akizungumza wakati akifunga Kikao Kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Rasilimaliwatu kutoka wizara, idara zinazojitegemea, wakala, taasisi na mashirika ya umma, sekretarieti za mikoa pamoja na mamlaka za serikali za mitaa kilichofanyika kwa siku tatu jijini Dodoma,
Na Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
NAIBU Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Ndege Qwaray, ametoa maagizo mazito kwa waajiri na wasimamizi wa watumishi wa umma nchini kuhakikisha wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi ili kuondoa malalamiko yanayowakabili watumishi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Akifunga Kikao Kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Rasilimaliwatu kutoka wizara, idara zinazojitegemea, wakala, taasisi na mashirika ya umma, sekretarieti za mikoa pamoja na mamlaka za serikali za mitaa kilichofanyika kwa siku tatu jijini Dodoma, Mhe.Qwaray amesema Serikali haitavumilia uzembe wa wasimamizi unaosababisha watumishi kunyimwa haki zao za msingi.
Amesema katika ziara zake mbalimbali amebaini changamoto nyingi za kiutumishi zinazotokana na kutofuata sheria na taratibu, ikiwemo ucheleweshaji wa upandishaji vyeo, kutolipwa kwa wakati stahili mbalimbali kama nauli za likizo na gharama za uhamisho, hali inayozalisha malalamiko miongoni mwa watumishi wa umma.
“Ni wajibu wa wasimamizi wa Utawala na Rasilimaliwatu kuwa kiungo muhimu kati ya viongozi na watumishi kwa kutoa ushauri sahihi unaozingatia sheria. Haki za watumishi lazima zilindwe wakati wote,” amesema Qwaray.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri huyo ameeleza kusikitishwa na baadhi ya waajiri na wasimamizi wanaoshindwa kuzingatia taratibu za uendeshaji wa mashauri ya nidhamu, jambo linalosababisha watumishi walioshtakiwa kushinda rufaa zao kutokana na dosari za kiutaratibu.
Amesema hali hiyo inaigharimu Serikali fedha nyingi pamoja na kuathiri taswira ya taasisi za umma mbele ya wananchi.
“Hii ni fedheha kubwa. Tunahitaji mashauri ya nidhamu yaendeshwe kwa kuzingatia sheria ili maamuzi yanayotolewa yawe halali na yenye kuhimili ukaguzi wa mamlaka za rufaa,” amesisitiza.
Mhe.Qwaray ametoa maelekezo kwa waajiri wote kutekeleza kwa wakati maamuzi yanayotolewa na Tume ya Utumishi wa Umma, akibainisha kuwa kutotekeleza maamuzi hayo ni ukiukwaji wa sheria na taratibu za utumishi wa umma.
Kuhusu mfumo wa e-Utendaji, amesema Serikali imebaini baadhi ya wasimamizi walishindwa kufanya tathmini za utendaji kazi kwa watumishi waliokuwa chini yao kwa mwaka wa utendaji wa 2024/2025, jambo lililosababisha baadhi ya watumishi kukosa sifa za kupandishwa vyeo licha ya kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Kutokana na hali hiyo, amemuelekeza Katibu Mkuu (Utumishi) kwa kushirikiana na waajiri wote kuwabaini wasimamizi waliozembea na kuwachukulia hatua za kinidhamu, ikiwemo kuwaondoa kwenye nafasi za uongozi pale itakapothibitika walishindwa kutekeleza wajibu wao bila sababu za msingi.
Aidha, amesema watumishi walioathirika kutokana na uzembe wa wasimamizi wao wanapaswa kupewa unafuu wa masharti ili wasiathirike katika maendeleo yao ya kiutumishi.
Katika eneo la maadili,Mhe.Qwaray ameeleza kuwa Serikali imebaini kuongezeka kwa matumizi ya lugha zisizofaa kwa wananchi, tuhuma za rushwa na matumizi yasiyo salama ya teknolojia katika baadhi ya taasisi za umma.
Kutokana na hali hiyo, ameagiza watumishi wote wa umma kujengewa uwezo kuhusu usalama wa taarifa za Serikali pamoja na matumizi sahihi ya teknolojia za Akili Unde (Artificial Intelligence), huku akisisitiza matumizi ya barua pepe rasmi za Serikali katika mawasiliano yote ya kikazi.
“Tunapaswa kulinda siri za Serikali na kuhakikisha matumizi ya teknolojia yanafanyika kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma,” amesema.
Akizungumzia umuhimu wa rasilimaliwatu, Qwaray amesema ndiyo nguzo kuu ya maendeleo ya taifa na kwamba usimamizi wake bora utasaidia kuongeza tija katika matumizi ya rasilimali nyingine za Serikali.
Aidha amewataka washiriki wa kikao hicho kutekeleza kwa vitendo maazimio yote yaliyofikiwa pamoja na maelekezo yaliyotolewa, na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wake Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kabla ya Julai 31, 2026.
Awali, Mhe.Qwaray amewapongeza washiriki wa kikao hicho kwa mijadala yao yenye tija na mchango walioutoa katika kujadili namna ya kuimarisha utawala na usimamizi wa rasilimaliwatu katika utumishi wa umma.
Amesema maarifa yaliyopatikana katika kikao hicho yanapaswa kutumika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi na kujenga utumishi wa umma wenye usikivu, uwajibikaji na matokeo chanya kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Juma Mkomi, amewapongeza waajiri wa taasisi mbalimbali za umma kwa kuwapa ruhusa na kuwawezesha watumishi wanaosimamia utawala na rasilimaliwatu kushiriki kikao kazi maalumu kilicholenga kuboresha utendaji katika Utumishi wa Umma.
Amesema kwa miaka ya hivi karibuni, utawala na usimamizi wa rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma umeendelea kuimarika kwa kiwango kikubwa kutokana na maboresho mbalimbali yanayotekelezwa na Serikali, ikiwemo matumizi ya mifumo ya kidijitali katika kusimamia watumishi na kuongeza uwajibikaji.
Hata hivyo, amebainisha kuwa pamoja na mafanikio hayo, bado kuna changamoto zinazohitaji kufanyiwa kazi ili kuhakikisha watumishi wanapata haki zao kwa wakati na taasisi za umma zinaendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.
“Tumepiga hatua kubwa katika usimamizi wa rasilimaliwatu, lakini bado zipo changamoto zinazohitaji ushirikiano wa pamoja kati ya waajiri, wasimamizi na watumishi wenyewe ili kuzitatua,” amesema Mhe. Mkomi.
Mkomi amesema kikao hicho kimetoa mapendekezo na maelekezo yatakayosaidia kuondoa vikwazo vinavyokwamisha maendeleo ya watumishi na kuimarisha usimamizi wa rasilimaliwatu katika sekta ya umma.