Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 15, 2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-Dodoma
Serikali imeendelea kuandika historia mpya katika Sekta ya Utalii nchini baada ya kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya utalii, hatua inayotajwa kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la kimataifa la utalii na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Hayo yamesemwa leo Mei 15, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Dkt.Kijaji amesema kuwa Serikali imekamilisha ujenzi wa viwanja vya ndege vitatu vya kisasa ndani ya maeneo ya hifadhi, ambapo kiwanja kimoja kimejengwa katika Nyerere National Park na viwanja viwili katika Ruaha National Park. Aidha, ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Mikumi unatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba mwaka 2026.
Hatua hiyo ameeleza kuwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kurahisisha usafiri wa watalii kutoka ndani na nje ya nchi, sambamba na kuongeza idadi ya wageni wanaotembelea vivutio vya utalii nchini.
“Serikali imekarabati viwanja vya ndege vinane katika hifadhi mbalimbali zikiwemo Mikumi National Park, Ruaha National Park, Nyerere National Park na Serengeti National Park ili kuongeza usalama na ubora wa huduma kwa wageni.”amesema Dkt.Kijaji
Katika juhudi nyingine za kuboresha mazingira ya utalii, jumla ya kilomita 3,757.92 za barabara pamoja na kilomita 523.14 za njia za watembea kwa miguu zimejengwa na kukarabatiwa katika maeneo yaliyohifadhiwa. Miundombinu hiyo inatarajiwa kurahisisha upatikanaji wa vivutio vya utalii huku ikiboresha uzoefu wa watalii wanaotembelea hifadhi hizo.
Aidha Wizara imeimarisha huduma za mapokezi na mapumziko kwa wageni kupitia ujenzi wa maeneo sita ya mapumziko na malango tisa ya kuingilia wageni katika hifadhi za Nyerere National Park, Mikumi National Park na Ruaha National Park.
Katika sekta ya uhifadhi wa misitu na ikolojia, vituo vya utalii pia vimejengwa katika misitu ya Meru, Vikindu, Mwambesi, Pindiro, Mlima Rungwe na Ziwa Duluti, huku kambi maalum ya watalii ikijengwa katika Hifadhi ya Misitu ya Mazingira Asilia ya Kilombero.
Katika hatua nyingine, juhudi hizo zimeendelea kuipa Tanzania heshima kimataifa, ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na Waziri wa Maliasili na Utalii, Ashatu Kijaji, walipokea Tuzo za World Travel Awards 2025 zilizotambua mchango wa Tanzania katika sekta ya utalii duniani.
Ukuaji huo wa miundombinu unatajwa kuwa ishara ya dhamira ya Serikali ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu kikubwa cha utalii barani Afrika na duniani kwa ujumla.