Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 15, 2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Sekta ya Maliasili na Utalii imeendelea kuonesha kuwa mhimili muhimu wa uchumi wa Taifa baada ya Wizara ya Maliasili na Utalii kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 989 ndani ya miezi kumi ya mwaka wa fedha 2025/2026, sawa na asilimia 83.45 ya lengo la makusanyo.
Hayo yamesemwa leo Mei 15, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027,amesema kuwa hatua hiyo ni ishara ya kuimarika kwa shughuli za utalii, uhifadhi wa maliasili pamoja na usimamizi wa rasilimali za taifa zinazochangia kwa kiwango kikubwa mapato ya Serikali.
Amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026 Wizara iliidhinishiwa kukusanya jumla ya Shilingi trilioni 1.18 kupitia taasisi mbalimbali zilizo chini yake.
“Kati ya fedha hizo, zaidi ya Shilingi bilioni 860 zilitarajiwa kukusanywa kupitia Tanzania National Parks Authority (TANAPA) na Ngorongoro Conservation Area Authority (NCAA) na kuwasilishwa katika Tanzania Revenue Authority (TRA).”amesema Dkt. Kijaji,
Aidha, zaidi ya Shilingi bilioni 115 zilipangwa kukusanywa kupitia Idara za Wizara, Mfuko wa Mambo ya Kale pamoja na Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA) kwa ajili ya Mfuko Mkuu wa Serikali.
Wizara ilitarajia kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 209 kupitia taasisi mbalimbali zinazotumia mfumo wa kidijitali wa MNRT Portal, hatua inayotajwa kuongeza uwazi na ufanisi katika ukusanyaji wa mapato.
Taasisi hizo ni pamoja na Tanzania Wildlife Research Institute (TAWIRI), Tanzania Forestry Research Institute (TAFORI), Tanzania Forest Services Agency (TFS), College of African Wildlife Management Mweka (CAWM) pamoja na taasisi nyingine za mafunzo, utafiti na utalii.
Amesema kuwa hadi kufikia Aprili 2026, TANAPA na NCAA zimeongoza kwa mchango mkubwa wa mapato baada ya kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 725, kiwango kinachoakisi kuongezeka kwa watalii na shughuli za uhifadhi nchini.
Wakati huo huo, Idara za Wizara, Mfuko wa Mambo ya Kale na TAWA zimekusanya zaidi ya Shilingi bilioni 85 huku taasisi zinazokusanya na kutumia kupitia mfumo wa MNRT Portal zikikusanya zaidi ya Shilingi bilioni 178.
Sekta hiyo imeendelea kuwa miongoni mwa sekta zenye mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania huku Serikali ikiweka mikakati zaidi ya kuongeza watalii, kuimarisha uhifadhi na kuvutia uwekezaji katika maeneo ya utalii na maliasili nchini.