Featured Kitaifa

TRILION 1.15 KUJENGA SHULE ZA MSINGI NA MADARASA MAPYA

Written by mzalendo

Serikali imetenga jumla ya Shilingi Trillion 1.15 kwa ajili ya kujenga shule mpya za msingi na madarasa mapya kwa kipindi cha miaka 5 ambapo kwa mwaka huu wa fedha Shule 302 mpya za msingi na madarasa zaidi ya 3000 zimejengwa.

Naibu Katibu Mkuu wa Tamisemi ( Elimu ) Dkt. Charles Msonde amesema hayo wakati akifungua Juma la Elimu Kitaifa wa mwaka 2024 ( GAWE) Mjini Geita na Serikali imefanya hivyo kwa ajili ya kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundisha.

Dkt. Msonde amesema katika jitihada za kuboresha elimu na miundombinu yake ambapo kwa upande wa shule za sekondari jumla ya Shilingi Trillion 1.2 zimetengwa kwa ajili ya kujenga shule mpya za sekondari 1026 na Kati ya hizo shule 26 zimetengwa mahususi kwa ajili ya wasichana za Mikoa za Bweni.

Kaimu Mkurugenzi Mtandao wa Elimu Nchini (TEN/MET) Martha Makala amesema Mkoa wa Geita umechaguliwa na wadau kwa ajili ya kuungana na wenyeji ili kuongeza nguvu katika kuhamasisha upatikanaji wa Elimu bora.

Afisa Elimu wa Mkoa wa Geita Anthony Mtweve amesema licha ya fedha wanazopewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya madarasa lakini bado kumekuwepo na msongamano wa wanafunzi katika madarasa na kupelekea miundombinu hiyo kutosheleza kwa muda mfupi kutokana kiwango kikubwa cha kuzaliwa watoto katika Mkoa huo.

Juma la Elimu Kitaifa 2024 (GAWE) imezinduliwa leo na inatarajiwa kufungwa siku ya Ijumaa ya wiki hii na Juma hili ina kauli mbiu isemayo “Elimu yenye kuleta Mabadiliko na iliyobora na Jumuishi”.

About the author

mzalendo