Na Mwandishi wetu, DAR ES SALAAM
MFUKO wa SELF Microfinance Fund umeendelea kujidhihirisha kuwa chombo muhimu katika kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia utoaji wa mikopo, bima na elimu ya fedha, hatua iliyomvutia Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, ambaye amepongeza mchango wa taasisi hiyo katika kuimarisha ujumuishi wa kifedha nchini.
Balozi Omar alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la SELF katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF), maarufu Sabasaba, leo Julai 2, 2026, ambapo alisema mfuko huo umeendelea kutekeleza kwa ufanisi jukumu lake la kuwafikia wananchi kwa huduma za kifedha na elimu inayowasaidia kutumia fursa za maendeleo.
SELF Microfinance Fund ni taasisi ya Serikali iliyo chini ya Wizara ya Fedha inayotoa huduma za mikopo, bima na elimu ya fedha kwa lengo la kuwawezesha wananchi, hususan wenye kipato cha chini, kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi.
Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa na mfuko huo, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara na Masoko wa SELF Microfinance Fund, Petro Mattaba, amesema taasisi hiyo hutoa mikopo kwa taasisi za huduma ndogo za fedha pamoja na mikopo ya moja kwa moja kwa wananchi.
Amesema mikopo inayotolewa kupitia taasisi za huduma ndogo za fedha husaidia kuwafikia wananchi waliopo maeneo ambayo SELF haiwezi kuyafikia moja kwa moja, hivyo kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa makundi mbalimbali.
Mattaba amesema walengwa wa mikopo ya moja kwa moja ni pamoja na watumishi wa umma, wafanyabiashara wadogo na wa kati, wakulima, wafugaji na wavuvi, ambao hupatiwa mitaji ya kuwawezesha kupanua shughuli zao za uzalishaji na biashara.
Ameongeza kuwa SELF ina matawi 12 Tanzania Bara na tawi moja Zanzibar, hatua inayorahisisha wananchi kupata huduma za mikopo, bima na ushauri wa kifedha katika maeneo mbalimbali nchini.
“Tumeshiriki Maonesho ya Sabasaba kwa lengo la kuwaelimisha wananchi kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na SELF, ikiwemo mikopo, bima na elimu ya fedha, ili waweze kutumia fursa hizo kuboresha maisha yao na kukuza shughuli zao za kiuchumi,” amesema Mattaba.
Ameeleza kuwa SELF ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki katika utekelezaji wa programu mbalimbali za Serikali zinazolenga kuwawezesha wananchi kiuchumi, zikiwemo programu za mikopo kwa vijana, wanawake na makundi mengine maalumu.
Mattaba amesema mwaka 2025 mfuko huo ulitoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 43 iliyowanufaisha zaidi ya wananchi 38,000 nchini, huku zaidi ya asilimia 51 ya wanufaika hao wakiwa wanawake.
Ameongeza kuwa SELF inaendelea kuzipatia taasisi za huduma ndogo za fedha mikopo yenye riba nafuu ili ziweze kuwafikia wananchi wengi zaidi, hususan waliopo vijijini na maeneo yenye upatikanaji mdogo wa huduma za kifedha.
Amewahimiza wananchi kutembelea banda la SELF katika Maonesho ya Sabasaba ili kupata elimu kuhusu huduma zinazotolewa na mfuko huo pamoja na kufahamu fursa mbalimbali za mikopo zinazoweza kuwasaidia kuboresha maisha na kuinua shughuli zao za kiuchumi.