Featured Kitaifa

MAMENEJA WA TARURA WAHIMIZWA KUFANYA UKAGUZI WA MIUNDOMBINU

Written by mzalendoeditor
Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) unaendelea na utekelezaji wa ujenzi na matengenezo ya miundombinu ili kuwawezesha wananchi kufanya shughuli zao za usafiri na usafirishaji kwa urahisi katika vipindi vyote vya mwaka.

………………………………….

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor H. Seff amewahimiza Mameneja wa TARURA wa Mikoa na Wilaya kufanya ukaguzi wa miundombinu hasa katika madaraja ya vyuma, barabara, makalavati pamoja na mitaro katika kipindi hiki cha mvua ili kuepusha madhara yanayoweza kuepukika na kuhakikisha barabara zinapitika.

Mhandisi Seff ameyasema hayo alipokuwa katika mahojiano maalum juu ya utekelezaji wa miradi ya TARURA ofisi kwake jijini Dodoma.

“Kwa sasa maeneo mengi mvua zinanyesha, Mameneja wa TARURA wa Mikoa wanatakiwa kufanya ukaguzi hasa kwenye madaraja ya chuma na kuchukua hatua stahiki ili kuzuia ajali zinazoweza kuepukika”, alisema Mhandisi Seff.

Mhandisi Seff ameyataja madaraja hayo ya chuma yaliyopo mkoani Songwe (Halmashauri ya Wilaya ya Momba), Mbeya (Halmashauri ya Wilaya ya Busokelo), Mara na maeneo mengine nchini kuwa yanatakiwa kufanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara ili kubaini kama kuna sehemu yenye changamoto ifanyiwe matengenezo ya haraka.

Pia, amewataka Mameneja wa Mikoa kuwasimamia Mameneja wa Wilaya kuhakikisha barabara zenye hali nzuri zinafanyiwa matengenezo ili zifikie umri wake ambao umepangwa na kuongeza kuwa katika kipindi hiki mvua zinapoendelea kunyesha mameneja waweze kutoa taarifa mapema kama kuna sehemu mawasiliano yamekatika ili matengenezo yafanyike kwa haraka.

Aidha, amewataka Mameneja wa Mkoa katika kipindi hiki cha mvua kufanya ukaguzi, na usafishaji wa mitaro pamoja na madaraja ili kuzuia maeneo ambayo maji yakiwa mengi yasiweze kuleta madhara kwenye miundombinu ya barabara pamoja na madaraja.

About the author

mzalendoeditor