Featured Kitaifa

RC MAKALLA AWAKABIDHI NSSF ENEO LA TOANGOMA LILILOVAMIWA NA WANANCHI.

Written by mzalendoeditor
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Amos Makalla amewataka Wananchi wote waliovamia na kujenga kwenye maeneo ya Mfuko wa hifadhi ya Jamii NSSF Kushirikiana na mfuko huo kwa kukubali kulipa fidia ya Fedha ili waweze kumilikishwa na kuendelea kusalia kwenye maeneo hayo.
RC Makalla ametoa maelekezo hayo Kufuatia Kamati iliyoundwa kuchunguza Mgogoro huo kubaini Wananchi hao walivamia maeneo ya NSSF na kujenga kinyume na sheria.
Akizungumza na Wavamizi hao wakati wa ziara ya utatuzi wa migogoro ya Ardhi Wilaya ya Temeke, RC Makalla ameelekeza NSSF kurasimisha upya maeneo hayo kwa kupima Viwanja ili Wavamizi waliotayari kulipa walipe na Baada ya Mgogoro kuisha Wananchi watapitiwa na Zoezi la anuani za Makazi na Kupatiwa namba.
Aidha RC Makalla amesema maamuzi hayo ni sehemu tu ya Busara ya Serikali ambapo ameonya tabia ya Wananchi kuvamia maeneo ya watu na Taasisi.
Miongoni mwa Viwanja vya NSSF Vilivyovamiwa vipo maeneo ya  Mwapemba, Toangoma na Mtoni Kijichi ambapo kwa eneo la Mwapemba zaidi ya Wananchi 100 wamevamia eneo la NSSF lenye ukubwa wa Mita za mraba 210,000 na kuweka Makazi.
Kwa upande wao baadhi ya Wavamizi akiwemo Rehema Mwita Wamemshukuru RC Makalla kwa uamuzi wa kuwaruhusu kulipa fidia ili waweze kusalia katika eneo Hilo na Wameahidi kutoa ushirikiano kwa NSSF Kulipa kiasi Cha fedha watakachotakiwa kulipa.

About the author

mzalendoeditor