Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 4,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Katika mwaka wa fedha 2026/27, Wizara imejipanga kutekeleza vipaumbele mbalimbali vinavyolenga kuimarisha sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kwa lengo la kuongeza ushindani wa Tanzania kitaifa na kimataifa.
Hayo yamebainishwa leo Mei 4 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Mhe.Makonda amesema kuwa moja ya maeneo makubwa ya kipaumbele ni kukamilisha ukarabati, uboreshaji na ujenzi wa miundombinu ya michezo nchini, sambamba na kuendelea kuitunza ili iwe endelevu na yenye viwango vya kimataifa.
“Wizara imejipanga kukamilisha maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji wa mashindano makubwa ya bara Afrika, AFCON 2027, yatakayofanyika kuanzia Juni hadi Julai 2027, tukio linalotarajiwa kuandika historia mpya kwa taifa.”amesema Mhe.Makonda
Aidha, Tanzania pia itakuwa mwenyeji wa Mashindano ya 74 ya Urembo ya Dunia Miss World 2027, tukio linalotarajiwa kuongeza mwonekano wa nchi kimataifa kupitia utalii, utamaduni na tasnia ya ubunifu.
Wizara pia imeweka mkazo katika kukamilisha na kuhuisha sera, sheria, mikakati, miongozo na kanuni mbalimbali zitakazosaidia kuimarisha usimamizi na utekelezaji bora wa sekta hizo muhimu.
Katika kukuza lugha na utamaduni, Serikali imejipanga kuimarisha na kustawisha matumizi ya Kiswahili kikanda na kimataifa, hatua inayolenga kuongeza ushawishi wa Tanzania katika mawasiliano ya kimataifa.
Kwa upande wa michezo, Wizara itaendelea kuziimarisha na kuzisaidia timu za taifa ili ziweze kushiriki kikamilifu katika mashindano mbalimbali ya kimataifa na kufanya vizuri, sambamba na kuboresha elimu na mafunzo katika tasnia za utamaduni, sanaa na michezo ili kukuza vipaji vya vijana.
Pia, Serikali imejipanga kuweka mazingira wezeshi yatakayoongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kukuza na kuendeleza sekta hizo, kwa lengo la kuongeza uwekezaji, ajira na ubunifu.
Vilevile, Wizara itaendelea kuratibu, kuendesha na kusimamia matamasha na matukio makubwa ya kitaifa na kimataifa katika sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kama njia ya kuitangaza Tanzania na kuimarisha uchumi wa sekta ya ubunifu.
Kwa ujumla, mipango hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kuijenga Tanzania yenye ushindani wa kimataifa, ubora wa miundombinu na mafanikio makubwa katika michezo na sekta za ubunifu.