WACHEZAJI watano wa Sudan wamekufa maji siku ya Jumatatu wakati mashua yao ilipozama kwenye mto Nile, kaskazini mwa mji mkuu Khartoum, shirika la habari la Suna liliripoti.
Wachezaji hao wa timu ya Navigation ya Ligi daraja la tatu walikuwa wakienda kucheza mechi wakati mashua yao ilipozama.
Shirika hilo la habari la Sudan halikufafanua jinsi chombo hicho kilizama, lakini kilisema wachezaji wote wa timu hiyo walikuwa ndani ya chombo hiko.
Timu hiyo ilikuwa ikisafiri kutoka mji wa Shendi katika jimbo la River Nile kaskazini mwa Sudan kuelekea mji wa Al Matama.
Ajali za boti kwenye Mto Nile ni jambo la kawaida, kwani vivuko vingi vya abiria ni vya zamani na si salama.
Matukio hutokea mara kwa mara wakati viwango vya maji vinapopanda na mikondo inakuwa na nguvu.