Na Edward Winchislaus
Bohari ya Dawa (MSD) imeweka bayana mafanikio na mwelekeo wake katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya nchini kupitia semina ya siku mbili kwa wahariri wa vyombo vya habari iliyofanyika jijini Dodoma.
Semina hiyo imelenga kuimarisha ushirikiano kati ya MSD na vyombo vya habari, sambamba na kutoa mrejesho wa utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo, huku wahariri wakipata fursa ya kujionea hali halisi ya utoaji huduma kupitia ziara katika vituo vya afya vya mikoa ya Dodoma, Singida na Pwani.
Akizungumza katika semina hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, amesema lengo kuu ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata bidhaa bora za afya kwa wakati, huku akisisitiza nafasi ya vyombo vya habari katika kufikisha taarifa sahihi kwa umma.
“Tunapokutana na wahariri tunapata nafasi ya kubadilishana uzoefu na kutoa mrejesho wa yale tuliyopanga na kuyatekeleza, lakini zaidi ni kuhakikisha jamii inaelewa juhudi zinazofanyika katika sekta ya afya,” amesema Tukai.
Amefafanua kuwa MSD ina jukumu la kuzalisha, kununua, kuhifadhi na kusambaza bidhaa za afya kwa hospitali, vituo vya afya na zahanati kote nchini, ambapo kwa sasa zaidi ya bidhaa 3,000 zipo katika mzunguko wa usambazaji.
Kwa mujibu wa Tukai, kiwango cha upatikanaji wa bidhaa za afya kupitia MSD kimefikia kati ya asilimia 81 hadi 83, huku mifumo ya ununuzi katika ngazi za mikoa ikisaidia kukamilisha mahitaji yaliyobaki ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa ufanisi zaidi.
Hata hivyo, amekiri kuwepo kwa changamoto ndogo katika baadhi ya maeneo, akieleza kuwa bado kuna kazi ya kufanya ili kufikia lengo la huduma jumuishi. “Unaweza kukuta wagonjwa 10, mmoja akakosa dawa; hiyo inaonesha bado tunapaswa kuongeza juhudi ili kufikia kila mmoja,” amesema.
Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, serikali imefanikiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa uhaba wa bidhaa za afya, ambapo kiwango cha upatikanaji kimeongezeka na kufikia wastani wa asilimia 80 kutokana na uwekezaji mkubwa katika miundombinu na rasilimali za sekta hiyo.
Kwa upande wao, wahariri walioshiriki semina hiyo wameeleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa, wakisema mafunzo hayo yamewawezesha kuelewa kwa kina hali halisi ya utoaji huduma za afya nchini.
Mwandishi wa habari wa EFM na TVE, Scolastica Mazura, amesema semina hiyo imewapa uwezo wa kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi zaidi kwa kuifikia jamii kwa taarifa sahihi. “Kupitia semina hii, tumeelewa kwa undani MSD ilipotoka, ilipo na inapokwenda, jambo linalotuwezesha kuandika na kusambaza taarifa sahihi kwa umma na kupunguza upotoshaji,” amesema Mazura.
Washiriki wengine wamepongeza uwekezaji wa vifaa tiba katika vituo vya afya walivyovitembelea, wakieleza kuwa umeboresha utoaji wa huduma, kupunguza msongamano wa wagonjwa na kuongeza imani ya wananchi katika sekta ya afya.
