Featured Kitaifa

WIZARA YA KATIBA NA SHERIA KUIMARISHA MSAADA WA KISHERIA KWA WANANCHI 2026/2027

Written by Alex Sonna
Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara hiyo  na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 24 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

WIZARA ya Katiba na Sheria  imeweka bayana mpango kazi wa kina kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ikilenga kuleta mageuzi makubwa katika Sekta ya Sheria kwa kuhakikisha huduma za haki zinawafikia wananchi hadi ngazi ya chini kabisa ya jamii.

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara hiyo  na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 24 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Dkt.Homera ameeleza  kuwa utekelezaji wa majukumu mbalimbali utaongozwa na lengo kuu la kujenga mfumo wa haki jumuishi, wenye ufanisi na unaoendana na mahitaji ya maendeleo ya Taifa.

Katika mwaka huo wa fedha, moja ya vipaumbele vikuu ni kusogeza huduma za msaada wa kisheria hadi ngazi ya msingi, hatua inayotarajiwa kuwasaidia wananchi wengi zaidi, hususan wasio na uwezo wa kumudu gharama za uwakili. Sambamba na hilo, Serikali itaweka mifumo endelevu ya kuhakikisha huduma hizo zinaendelea kupatikana kwa ufanisi kote nchini.

Aidha amesema kuwa Wizara  imepanga kuandaa Sera ya Taifa ya Haki Madai pamoja na Mpango Kabambe wa Sekta ya Sheria, nyaraka ambazo zinatarajiwa kuweka mwelekeo mpya wa uendeshaji wa masuala ya kisheria nchini.

Katika kuongeza uelewa wa wananchi, elimu kuhusu Sera ya Taifa ya Haki Jinai na Msaada wa Kisheria itatolewa kwa wadau mbalimbali, huku viongozi, watendaji na umma kwa ujumla wakipewa elimu ya Katiba na uraia ili kuimarisha utawala bora na uwajibikaji.

Aidha, Serikali itaendelea kutekeleza mipango ya haki za binadamu, ikiwemo Mpango Kazi wa Kitaifa wa Haki za Binadamu pamoja na mkakati wa elimu ya haki hizo, hatua inayolenga kulinda hadhi na haki za kila Mtanzania.

Katika kupunguza migogoro mirefu mahakamani, Wizara itaongeza nguvu katika matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro, huku pia ikiimarisha ushirikiano wa kimataifa kupitia uandaaji wa mikataba ya kusafirisha watuhumiwa kati ya nchi na nchi.

Sekta ya maliasili nayo haijaachwa nyuma, ambapo maafisa kutoka taasisi mbalimbali watajengewa uwezo wa kusimamia rasilimali za taifa kwa ufanisi zaidi, kulinda utajiri asilia na kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi.

Kwa upande wa huduma za kijamii, Wizara itaimarisha usimamizi wa mirathi na mali za wadhamini, pamoja na kuhamasisha wananchi kuandika na kusajili wosia ili kuepuka migogoro ya kifamilia inayotokana na urithi.

Hatua nyingine muhimu ni kuanzishwa kwa rejista ya watoa huduma za ufilisi, itakayosaidia kuweka uwazi na ufanisi katika kushughulikia masuala ya kifedha na mali za wadaiwa.

Ili kuendana na mabadiliko ya kisasa, Wizara pia imepanga kutoa mafunzo ya ubobezi kwa wataalam wa sheria katika maeneo ya kimkakati, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kuharakisha mageuzi ndani ya sekta hiyo.

Kwa upande wa Mahakama, Tume ya Utumishi wa Mahakama imejipanga kuimarisha mifumo ya TEHAMA katika usimamizi wa ajira, maadili na nidhamu ya watumishi, pamoja na kuboresha uteuzi na kuongeza uwezo wa taasisi kutoa huduma bora.

Aidha, jitihada zitaelekezwa katika kuimarisha nidhamu na maadili ya watumishi wa Mahakama, pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu ya taasisi hiyo ili kuongeza uwazi na imani ya wananchi.

Kwa ujumla, mpango huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuijenga upya sekta ya sheria kwa vitendo kwa kuisogeza karibu na wananchi, kuifanya iwe ya kisasa na kuhakikisha haki inakuwa siyo nadharia, bali uhalisia kwa kila Mtanzania.

About the author

Alex Sonna