Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara hiyo na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 24 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeweka wazi dira mpya ya mageuzi ya Sekta ya Sheria kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ikilenga kuifanya sekta hiyo kuwa mhimili mkuu wa maendeleo ya uchumi, badala ya kubaki kuwa mtoa huduma wa kawaida wa haki.
Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara hiyo na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 24 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.
Dkt.Homera amesema kuwa Serikali inalenga kujenga mfumo wa sheria unaotoa haki kwa wakati, wenye ufanisi, unaotumia teknolojia za kisasa na unaochochea uwekezaji na ukuaji wa uchumi wa Taifa.
“Lengo letu siyo tu kutoa haki, bali kuifanya sekta ya sheria kuwa injini ya maendeleo ya kiuchumi,”amesmea Dkt.Homera
Amesema kuwa wizara imeainisha maeneo 15 ya kimkakati yatakayoongoza utekelezaji wa mpango huo. Miongoni mwa vipaumbele vikuu ni pamoja na kuimarisha Katiba ili iwe chombo hai kinachochochea utawala bora, pamoja na kupanua huduma za haki hadi ngazi za vijiji na kata ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Serikali pia imepanga kuongeza nguvu katika utoaji wa msaada wa kisheria kupitia Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (MSLAC), ambayo sasa inaingia awamu ya pili kwa lengo la kuwafikia Watanzania wote bila kujali hali zao za kiuchumi au kijiografia.
Katika hatua ya kulinda haki na usalama wa wananchi, Wizara imepanga kuanzisha mfumo maalum wa ulinzi wa mashahidi na watoa taarifa za uhalifu, hatua inayotarajiwa kuongeza ujasiri wa wananchi kushiriki katika mapambano dhidi ya uhalifu.
Aidha, matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR) yataimarishwa zaidi ili kupunguza mlundikano wa kesi mahakamani, huku mifumo ya kidijitali ikiwekewa msukumo mkubwa ili kurahisisha utoaji wa huduma za kisheria.
Katika kuendana na mahitaji ya dunia ya kisasa, Wizara pia inalenga kuboresha ubora wa utungaji wa sheria, kuimarisha taasisi za utawala bora pamoja na kuongeza uwezo wa wataalam wa sheria kupitia mafunzo ya ubobezi.
Hatua nyingine muhimu ni kuimarisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wakili Mkuu wa Serikali pamoja na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka ili ziweze kushughulikia kwa ufanisi mashauri ya kimataifa na kulinda maslahi ya taifa katika uwekezaji na mikataba ya kimataifa.
Kwa upande wa uwajibikaji, Serikali imeweka mkazo katika kuimarisha nidhamu ndani ya taasisi za umma, kupambana na rushwa na kuhakikisha matumizi sahihi ya madaraka.
Mpango huo pia unalenga kuimarisha usimamizi wa mali za wadhamini wa umma, pamoja na kuboresha huduma za mirathi na ufilisi ili kulinda haki za wanufaika.
Katika kuonesha dhamira ya dhati, Serikali imesisitiza kuwa utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (MSLAC II) hautakuwa wa kawaida, bali ni mageuzi ya msingi yatakayobadili mfumo mzima wa utoaji haki nchini.
Kupitia mpango huo, Serikali inalenga kujenga mfumo jumuishi unaounganisha Serikali Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa, wadau wa maendeleo pamoja na jamii ili kuhakikisha hakuna Mtanzania anayenyimwa haki.
Kwa mwelekeo huu mpya, Tanzania inaingia katika sura mpya ya mfumo wa sheria mfumo unaolenga si tu kusimamia haki, bali pia kujenga taifa lenye usawa, uwajibikaji na maendeleo endelevu kuelekea mwaka 2050.