Featured Kitaifa

SERIKALI YANG’ARA MAHAKAMANI: YASHINDA ZAIDI YA ASILIMIA 88 YA MASHAURI, YAOKOA MABILIONI YA FEDHA ZA UMMA

Written by Alex Sonna

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara hiyo  na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 24 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

Serikali imeendelea kuonesha uimara wake katika kulinda maslahi ya taifa kupitia usimamizi madhubuti wa mashauri ya madai na usuluhishi, huku mafanikio makubwa yakirekodiwa katika kipindi cha miezi tisa kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 24 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Dkt.Homera ameeleza  kuwa kupitia Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, juhudi zimeelekezwa katika kuratibu, kusimamia na kuiwakilisha Serikali katika mashauri mbalimbali ndani na nje ya nchi. Lengo kuu likiwa ni kuhakikisha rasilimali za umma zinalindwa na haki inapatikana kwa ufanisi.

Katika kipindi hicho, jumla ya mashauri ya madai 10,401 yaliendeshwa ongezeko la asilimia 15.4 ikilinganishwa na mashauri 9,013 ya mwaka uliopita. Kati ya mashauri hayo, 9,663 yalikuwa ya kitaifa, 34 ya kimataifa, na 704 yakihusu masuala ya kikatiba na haki za binadamu.

 “Mashauri 641 yalihitimishwa, ambapo Serikali ilishinda mashauri 565 sawa na asilimia 88.1 ya mashauri yote yaliyomalizika. Mafanikio hayo yameiwezesha Serikali kuokoa zaidi ya shilingi bilioni 316 ambazo zingelipwa endapo ingetoka kushindwa katika kesi hizo.”amesema Dkt.Homera 

Kati ya fedha hizo, zaidi ya shilingi bilioni 313 zilitokana na ushindi katika mashauri yaliyosikilizwa mahakamani, huku zaidi ya shilingi bilioni 2.8 zikiokolewa kupitia majadiliano ya nje ya mahakama ikiashiria umuhimu wa njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Katika uwanja wa kisiasa, Ofisi hiyo ilisimamia mashauri 76 ya uchaguzi yaliyopinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025. Kati ya hayo, mashauri 39 yaliyomalizika Tanzania Bara, Serikali ilishinda yote, huku mengine yakiendelea kusikilizwa katika mahakama mbalimbali Bara na Zanzibar.

Aidha, mashauri 13 ya mapitio ya kimahakama yaliwasilishwa, yakihusiana na mchakato wa uchaguzi, ingawa hayakulenga moja kwa moja kupinga matokeo ya ubunge au udiwani.

Kwa upande wa usuluhishi, mashauri 251 yaliendeshwa, ikiwa ni ongezeko la asilimia 20.1 kutoka mwaka uliopita. Kati ya hayo, 221 yalikuwa ya ndani na 30 ya kimataifa. Mashauri 18 yalihitimishwa, na kuiwezesha Serikali kuokoa zaidi ya shilingi bilioni 6.8 pamoja na dola za Marekani zaidi ya milioni 418.

Hatua hizi zinaakisi mkakati wa Serikali wa kuimarisha matumizi ya majadiliano na maridhiano kama njia mbadala ya kupunguza gharama na muda wa mashauri.

Katika kuzuia migogoro kabla haijafika mahakamani, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilifanyia kazi notisi 765 za siku 90 zilizowasilishwa na wadai waliokuwa na nia ya kuishtaki Serikali. Kupitia majadiliano na taasisi husika, baadhi ya migogoro hiyo ilimalizika kwa muafaka bila kufikishwa mahakamani.

Mbinu hiyo, inayozingatia falsafa ya 4R (Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Ujenzi Mpya), imeisaidia Serikali kuepuka gharama kubwa za riba, faini na fidia ambazo zingetokana na kushindwa kwa mashauri.

Kwa mwenendo huu, ni wazi kuwa Serikali inaendelea kujijengea taswira ya taasisi inayosimamia sheria kwa umakini, huku ikiweka mbele maslahi ya wananchi na maendeleo endelevu ya Taifa.

About the author

Alex Sonna