Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 17,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeendelea kuimarisha mikakati yake ya muda mrefu katika sekta ya madini kwa kutangaza utekelezaji wa maeneo mapya ya kipaumbele kwa mwaka wa fedha 2026/2027, yakiongozwa na dira ya “Mining Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri” inayolenga kuifanya sekta hiyo kuwa mhimili mkuu wa uchumi wa Taifa.
Hayo yamesemwa leo Aprili 27, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Akiwasilisha mpango huo bungeni,Mhe.Mavunde amesema kuwa dira hiyo inalenga kuhakikisha rasilimali za madini zinasimamiwa kwa ufanisi na uendelevu, huku zikichangia kwa kiwango kikubwa katika pato la taifa na kuboresha maisha ya wananchi.
” Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) imepanga kuongeza kasi ya tafiti za kina za jiosayansi, zikiwemo tafiti za kisasa za jiofizikia kwa kutumia teknolojia ya angani. Lengo ni kuongeza uelewa wa rasilimali zilizopo kutoka asilimia 16 ya sasa hadi kufikia asilimia 34, huku matarajio yakiwa kufikia angalau asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.”amesema
Waziri huyo ameeleza kuwa upatikanaji wa taarifa sahihi za jiolojia utafungua milango ya uwekezaji zaidi na kuchochea ukuaji wa sekta nyingine muhimu kama viwanda, kilimo, ujenzi na huduma za kifedha.
Katika kuimarisha ushiriki wa wananchi, Serikali inaendelea kutekeleza programu ya Mining for a Brighter Tomorrow (MBT), inayolenga kuwawezesha wachimbaji wadogo, hususan vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum. Programu hiyo inatarajiwa kuongeza ajira, kipato na ushiriki wa makundi hayo katika uchumi jumuishi kupitia sekta ya madini.
Sambamba na hilo, Wizara imeweka mkazo katika kuendeleza rasilimali watu kwa kuwajengea uwezo wataalamu wa sekta ya madini kupitia mafunzo ya ndani na nje ya nchi. Mafunzo hayo yatahusisha maeneo muhimu kama ukadiriaji wa rasilimali, uchambuzi wa kifedha, uthaminishaji wa madini na teknolojia za uongezaji thamani.
Katika kuendana na maendeleo ya teknolojia, Serikali pia inakamilisha ujenzi wa mfumo wa kisasa wa kidijitali wa usimamizi wa sekta ya madini (MSMIS). Mfumo huo utarahisisha upatikanaji wa taarifa, kuongeza uwazi na kuboresha ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa kuunganisha mifumo mbalimbali ya kidijitali.
Kwa upande wa mazingira, Serikali imeweka mkakati maalum wa kuhakikisha shughuli za madini zinafanyika kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Kupitia Mpango Kazi wa Mazingira wa Sekta ya Madini wa mwaka 2025–2030, kanuni za kimataifa za mazingira, jamii na utawala bora (ESG) zitaingizwa kikamilifu katika shughuli zote za madini.
Kwa ujumla, utekelezaji wa mipango hiyo unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya madini, kuongeza uwekezaji, ajira na mapato, na hatimaye kuimarisha uchumi wa Taifa kwa manufaa ya Watanzania wote.