WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameelekeza fedha zilizokuwa zimepangwa kugharamia maadhimisho ya Sherehe za Muungano mwaka huu, zitumike kukarabati miundombinu ya barabara iliyoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha nchini.
Ameyasema hayo, leo Jumatatu, Aprili 20, 2026 Ofisini kwake Mlimwa Jijini Dodoma alipokuwa akiuarifu umma kuhusu maadhimisho ya Miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yatakavyofanyika.
“Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 62 ya Muungano yatafanyika katika ngazi ya Mikoa yote nchini ambapo Viongozi Wakuu wa Kitaifa watafanya shughuli za kutembelea, kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi ya maendeleo” Amesema Dkt. Mwigulu.