Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Fransis Olwero, amesema maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka 2026 yamekuwa jukwaa muhimu kwa taasisi hiyo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa matumizi sahihi ya vipimo katika shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Akizungumza na waandishi wa habari Juni 23, 2026, katika banda la WMA kwenye maadhimisho hayo yanayoendelea jijini Dodoma, Olwero alisema wananchi wengi waliotembelea banda hilo wamepata fursa ya kujifunza kuhusu nafasi ya vipimo katika maisha ya kila siku na maendeleo ya uchumi.
Alisema matumizi ya vipimo sahihi ni jambo la msingi kwa kuwa sehemu kubwa ya shughuli za kila siku nchini hutegemea vipimo, kuanzia biashara, kilimo, viwanda hadi huduma mbalimbali. Alisisitiza kuwa uelewa wa matumizi sahihi ya vipimo husaidia kuongeza uwazi, ufanisi na haki katika shughuli za kiuchumi.
Olwero alieleza kuwa WMA imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi, wawekezaji na watumishi wa umma waliotembelea banda hilo, huku wengi wao wakionesha kufurahishwa na maarifa waliyopata kuhusu umuhimu wa kuzingatia viwango vya vipimo vinavyotambulika kisheria.
Katika sekta ya kilimo, alisema ni muhimu kwa wakulima na wafanyabiashara kutumia vipimo sahihi wakati wa kununua na kuuza mazao badala ya kutegemea makadirio au magunia yasiyo na viwango rasmi, hali inayoweza kusababisha hasara na migogoro katika biashara.
Aliongeza kuwa matumizi ya mfumo wa vipimo sahihi yatachangia kuondoa vitendo vya udanganyifu katika biashara ya mazao, hasa katika kipindi cha mavuno ambapo biashara nyingi hufanyika kwa wingi.
Kwa mujibu wa Olwero, matumizi ya vipimo vinavyokubalika kisheria yataongeza uaminifu kati ya wanunuzi na wauzaji, sambamba na kujenga mazingira bora ya biashara yenye ushindani wa haki.
Aidha, aliwataka wakulima, wanunuzi na madalali kuendelea kuzingatia matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli zao ili kuhakikisha biashara inafanyika kwa uwazi na kuwanufaisha pande zote zinazohusika.
Alisisitiza kuwa sheria za vipimo zipo na zinaelekeza matumizi sahihi ya vipimo nchini, akionya kuwa mtu yeyote atakayekiuka taratibu na masharti yaliyowekwa atachukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.
