Serikali imeendelea kusisitiza ushiriki jumuishi wa wanawake, vijana na makundi yenye mahitaji maalum katika utafiti, sayansi, teknolojia na ubunifu ili kuongeza mchango wao katika maendeleo ya taifa.
Kauli hiyo imetolewa Juni 12, 2026 jijini Dodoma na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, wakati wa ufunguzi wa Warsha ya kuwajengea uwezo Wadau kuhusu Utekelezaji wa Kiunzi cha Kitaifa cha Usawa na Haki za Kijinsia katika Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STU).
Ameeleza kuwa kwa sasa wanawake ni takribani asilimia 36 ya watafiti nchini, huku wasichana wakichangia zaidi ya asilimia 45 ya wanafunzi wapya wa masomo ya STEM vyuoni katika mwaka wa fedha 2023/24.
Ameongeza kuwa vijana walio chini ya miaka 35 wamechangia karibu asilimia 40 ya miradi iliyoidhinishwa na COSTECH katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Katibu Mkuu Nombo amesisitiza kuwa taasisi za utafiti na ubunifu zinapaswa kutumia kikamilifu kiunzi hicho katika sera, mipango na bajeti zao ili kuhakikisha matokeo ya tafiti na bunifu yananufaisha wananchi wote na kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa.
“Nchi yetu imeendelea kutambulika kimataifa katika kuisimamia na kuendeleza usawa wa kijinsia chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye alichaguliwa kuwa Kinara wa kuendeleza ajenda hii, sisi kama wadau wa STU tunapaswa kuunga mkono maono haya na kuhakikisha yanazingatiwa katika shughuli zote za maendeleo ya Taifa” amesema Prof. Nombo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, Prof. Ladislaus Mnyone, amesema ushiriki wa makundi yote ni muhimu ili juhudi za nchi ziwe na matokeo ya pamoja na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa haraka zaidi.
Naye, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Katare Bugwesa, amebainisha kuwa kiunzi hicho kinalenga kuongeza ushiriki wa wanawake katika maamuzi, kuimarisha maendeleo yao kitaaluma na kujumuisha masuala ya kijinsia katika tafiti na bunifu.
