Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imezindua rasmi mpango wa kihistoria wa ukopeshaji wa majiko ya umeme kwa wateja wa TANESCO na mradi wa ujenzi wa vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme, hatua inayolenga kuharakisha matumizi ya nishati safi nchini na kupunguza gharama za maisha kwa wananchi.
Akizungumza leo Juni 11,2026 jijini Dodoma wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amesema Tanzania imefikia hatua mpya ya maendeleo ambapo umeme hautatumika kwa kuwasha taa pekee, bali utakuwa nyenzo muhimu ya kuboresha maisha ya wananchi kupitia kupikia na usafiri.
Dkt. Deogratius Ndejembi,
Mhe.Ndejembi amesema mpango huo utawezesha wananchi kupata majiko ya umeme yaliyoidhinishwa kwa mkopo na kurejesha fedha kidogo kidogo kupitia manunuzi ya umeme wa LUKU, jambo litakaloondoa kikwazo cha gharama za awali za ununuzi wa majiko.
“Tunamwondolea mwananchi kikwazo kikubwa kilichokuwa kinamzuia kuingia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia. Kwa mara ya kwanza duniani, Tanzania inatekeleza mfumo wa On-Bill Financing ambapo gharama za jiko zitalipwa taratibu kupitia matumizi ya umeme,” amesema Mhe. Ndejembi.
Amebainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024–2034 unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, huku asilimia 20 wakitumia umeme kupikia.
Waziri huyo amesema mafanikio ya mpango huo yamechochewa na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sekta ya umeme, ambao umeongeza uzalishaji wa nishati na kufikisha zaidi ya megawati 4,000.
Amesema kukamilika kwa Mradi wa Umeme wa Julius Nyerere wenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 kumetoa uhakika wa umeme wa kutosha, hivyo hatua inayofuata ni kuongeza matumizi yenye tija ya nishati hiyo katika shughuli za kila siku za wananchi.
Katika hatua nyingine, TANESCO imezindua kituo chake cha kwanza cha kuchajia magari ya umeme, ikiwa ni mwanzo wa utekelezaji wa mradi wa kufunga mashine 50 za kisasa za kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme katika ofisi zake za mikoa yote nchini.
Mhe.Ndejembi amesema mradi huo umefadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa ushirikiano na kampuni ya AUTEL, inayotengeneza mifumo ya kisasa ya kuchajia magari ya umeme.
“Tunazindua si mashine pekee ya kuchajia magari, bali mfumo mpya wa usafiri nchini. Huu ni mwanzo wa safari ya kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa vinara wa matumizi ya usafiri wa umeme katika Afrika Mashariki,” amesema.
Ameongeza kuwa kuanzishwa kwa vituo hivyo kutapunguza gharama za usafiri, kuongeza imani kwa wawekezaji na watumiaji wa teknolojia za usafiri wa umeme, pamoja na kuchochea uwekezaji mpya katika uchumi wa kijani.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, matumizi ya kuni na mkaa bado ni tishio kubwa kwa mazingira, ambapo zaidi ya hekta 469,000 za misitu hupotea kila mwaka kutokana na mahitaji ya nishati hizo.
Amesema matumizi ya majiko ya umeme yatachangia kupunguza uharibifu wa mazingira, kulinda afya za wananchi dhidi ya madhara ya moshi na kuokoa maisha ya wanawake na watoto ambao wamekuwa waathirika wakubwa wa matumizi ya nishati zisizo safi.
Katika kuhakikisha wananchi wananufaika na miradi hiyo,Ndejembi ameiagiza TANESCO kusambaza huduma za ukopeshaji wa majiko katika maeneo yote nchini, kuongeza elimu kuhusu matumizi ya umeme kupikia na kuhakikisha vituo vya kuchajia vinakamilika kwa wakati.
Pia amewataka wananchi kuchangamkia fursa hiyo ya mikopo ya majiko yenye masharti nafuu, huku akitangaza kuwa kwa siku 30 za mwanzo wananchi watapata huduma za kuchaji vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme bure kabla ya kuanza kutozwa gharama nafuu.
“Miaka ijayo tutakapoandika historia ya mapinduzi ya nishati safi nchini, tutakumbuka kuwa safari hii ilianza pale tulipoamua kuupeleka umeme jikoni na barabarani. Hapo ndipo tulipoamua kuufanya umeme kuwa sehemu ya maisha ya kila Mtanzania,” amesema Mhe. Ndejembi.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO),Bw. Lazaro Twange, amesema shirika hilo limejipanga kukopesha majiko ya umeme milioni moja kwa wateja wake ndani ya kipindi cha miaka mitatu ili kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Twange amesema TANESCO inaendelea kukua kwa kasi na kufikia wateja takribani milioni 6.5, huku pia ikiwa na uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 4,000 za umeme kufuatia uwekezaji mkubwa wa serikali katika sekta ya nishati.
Ameeleza kuwa mpango huo tayari umeanza kutekelezwa kupitia ufadhili kutoka Uingereza, ambapo wateja wapya 1,032 tayari wamepata majiko ya umeme kwa mkopo.
Aidha, amesema matumizi ya umeme yanapaswa kupanuka zaidi ya matumizi ya kawaida ya nyumbani na kujumuisha kupikia pamoja na kuendesha vyombo vya usafiri kama treni, magari, bajaji na pikipiki, ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na ajenda ya nishati safi nchini.