WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuondoa vikwazo na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.
Ameyasema hayo leo (Jumatano, Juni 10, 2026), wakati akizindua ghala la forodha la kampuni ya Ciwaye Trading Co. Ltd Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.
“Kama tunavyoheshimu sekta ya umma, tunatakiwa kuheshimu sekta binafsi kwa uzito ule ule, kama mataifa mengine yaliyoendelea, uchumi wa mataifa hayo nguzo yake ni sekta binafsi.”
Dkt. Mwigulu aliongeza kwa kusema “Kwa kuheshimu hilo, nimeona nije kuzindua mradi huu, kama ambavyo nimepita kwenye ziara kuzindua miradi ya Serikali, ndiyo maana nimeona na hapa nije mwenyewe.”
Aidha, ameeleza kuwa mradi huo una umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo hauna budi kulelewa.
“Ukubwa wa jambo hili haupimwi kwa majengo, bali kwa uthubutu na matokeo yanayoakisi Dira yetu ya maendeleo na maono ya Rais wetu ya kuhakikisha mradi kama huu unatoa matokeo yaliyokusudiwa.” Amesisitiza Waziri Mkuu Mwigulu.
Waziri Mkuu ameongeza kuwa mradi huo unatazamwa na Serikali kama mradi wa kielelezo wa kutekeleza Dira 2050 na ndiyo maana Serikali imekuwa ikiboresha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo maboresho ya sheria za uwekezaji.
“Zimebadilishwa Sheria za uwekezaji ili kuhakikisha wazawa wananufaika na kuushika uchumi, zamani vivutio vya uwekezaji viliwanufaisha wageni, lakini sasa wazawa wanapata vivutio hivyo,” ameeleza Waziri Mkuu.
Ameongeza kuwa: “Mfano katika sekta ya uzalishaji, zamani miradi yote mikubwa ilikuwa inatekelezwa na wageni, lakini mabadiliko hayo ya sheria yamewezesha wazawa kutekeleza miradi mikubwa, na sasa wanaweza kuajiri wageni katika utekelezaji wa miradi hiyo.”
Waziri Mkuu Mwigulu amesema mkakati mwingine unaoenda sambamba na mabadiliko ya sheria, ni pamoja na kuondoa zaidi ya tozo 270 ili kuwapunguzia mzigo wafanyabiashara na walaji wa mwisho.
Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu ameeleza kufurahishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wake, kwani umetekelezwa ndani ya muda mfupi lakini viwango vya ubora vimezingatiwa.
Amesema uamuzi wa kuanzisha ghala hilo mkoani Dodoma ni wa kimkakati kwani Dodoma ipo katikati ya nchi, ikiunganisha maeneo mengine ya nchi na fursa zilizopo katika maeneo hayo, ambapo amewataka wafanyakazi wa mradi huo kuwa waaminifu ili mradi uwe na faida endelevu, kwao binafsi na jamii.
Pia Waziri Mkuu Mwigulu amewahimiza Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhamasisha wawekezaji kuwekeza kwenye mikoa na maeneo yao kwa kuweka miundombinu inayochochea vyanzo vya mapato na kukua kwa uchumi.
Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dk. Rajab Seif, amesema mwekezaji huyo ametoa fursa za ajira kwa wananchi wa Chamwino na Mkoa wa Dodoma kwa ujumla.
Amesema TAMISEMI kupitia Halmashauri ya Chamwino itaendelea kumpatia mwekezaji huyo ushirikiano wa kutosha.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ameeleza kuwa katika vipaumbele vya kukuza uchumi kwenye mkoa huo ni uwepo wa mji wa kimkakati.
Amesema uwepo wa ghala hilo ni kutafsiri maono ya mkoa huo kuufanya kuwa mji wa kimkakati kama kiungo muhimu kibiashara kutoka ndani na nje ya nchi.
“Dodoma inafikika kwa pande zote. Tunafahamu SGR inafika Dodoma, tuna uwanja wa ndege wa kimataifa ambao huenda mwaka huu tukashuhudia ndege kutoka nje ya nchi kutua.
Ameongeza: “Tunashuhudia utekelezaji wa maono haya. Tunatamani kuona Mkoa wa Dodoma tunatoa mchango kwenye pato la taifa na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja.”
Mkurugenzi wa Kampuni ya Ciwaye Trading, Happy John, amesema kampuni hiyo itaendesha shughuli zake kwa kuzingatia sheria za forodha, utunzaji mizigo kwa uwazi na ulipaji kodi.
Vilevile, amesema kampuni hiyo itachangia kutoa ajira kwa wananchi, hivyo iliiomba serikali kutengewa eneo maalumu kwa ajili ya ujenzi wa bandari kavu mkoani Dodoma.
Amesema uwepo wa bandari hiyo utapunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam, kuongeza uwezo wa reli ya SGR kusafirisha mizigo na kuifanya Dodoma kuwa kitovu kikuu cha usafirishaji mizigo.
“Tunamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini,” amesisitiza.
Mwakilishi wa Kaminsha Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambaye ni Naibu Kamishna wa Forodha, Wahabi Matengo, amesema uzinduzi huo wa ghala la kwanza la forodha Dodoma itahamasisha jamii kulipa kodi kwa hiyari.
Amesema kampuni hiyo imekidhi vigezo kuanzisha ghala hilo la forodha ambalo ni nyenzo muhimu katika kuongeza mapato ya serikali.
“Ghala hili limeidhinishwa pia kuhifadhi magari makubwa na mitambo mpaka yatakapokidhi matakwa ya forodha kwa kulipa kodi stahiki,” amesisitiza.
Pia, amesema maghala ya forodha yanakuza biashara za kimataifa kwa kuruhusu bidhaa zinazohifadhiwa kuuzwa nje ya nchi na kuongeza wigo wa upatikanaji bidhaa kwa wakati.
Matengo amesema TRA itahakikisha shughuli zote zinafanyika kwa mujibu wa sheria ili kuhakilisha ghala hilo linachangia mapato na maendeleo ya mkoa huo.
Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Janeth Mayanja, amesema uwekezaji huo utaongeza fursa kwa wananchi wa wilaya hiyo.








