Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
WAKALA wa Vipimo Tanzania (WMA) Mkoa wa Dodoma umewataka wananchi na wafanyabiashara kuhakikisha wanatumia vipimo sahihi katika shughuli za biashara ili kulinda maslahi ya wanunuzi na kuongeza ufanisi wa biashara nchini.
Hayo yameelezwa leo Mei 19,2026 jijini Dodoma na Meneja wa WMA Mkoa wa Dodoma, Saidi Ibrahimu, wakati wa kukabidhi mizani iliyohakikiwa na wakala huo kwa wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Vipimo Duniani ambayo huadhimishwa Mei 20 kila mwaka.
Amesema matumizi ya mizani na vipimo vilivyohakikiwa ni muhimu katika kujenga mazingira ya biashara yenye haki na ushindani, huku akisisitiza kuwa wakala huo utaendelea kufanya ukaguzi wa kushtukiza katika maeneo ya uzalishaji, maghala na masoko mbalimbali.
“Matumizi ya vipimo visivyo sahihi yamekuwa chanzo cha wafanyabiashara wengi kupata hasara bila kutambua, huku wananchi wakipunjwa kwa kuuziwa bidhaa pungufu ya kiwango wanachostahili kupata.”amesema Bw.Ibrahimu
Aidha, Ibrahimu ameonya kuwa mfanyabiashara atakayebainika kutumia mizani au vipimo visivyo sahihi atachukuliwa hatua za kisheria, ikiwemo kutozwa faini ya Sh milioni 20, kifungo kisichopungua miaka miwili jela au adhabu zote kwa pamoja.
Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wafanyabiashara wa Soko la Majengo, Fred Segamang’ombe, ameishukuru WMA kwa kutoa mizani kwa baadhi ya wanawake wafanyabiashara katika soko hilo, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza tija na faida katika biashara zao.
Amesema wafanyabiashara wengi sokoni hapo wamekuwa wakikosa mizani na hivyo kutumia makopo au kupanga bidhaa chini, hali inayochangia kuuza bidhaa kwa hasara.
“Wafanyabiashara wengi hununua mzigo uliopimwa kwa uzito rasmi, lakini wanapouza hutumia makopo, mifuko au kupanga bidhaa chini bila kipimo sahihi. Mwisho wa siku wanajikuta wanapata hasara na kuingia kwenye madeni,” amesema
Segamang’ombe amesema Soko la Majengo lina takribani wafanyabiashara 4,000, ambapo asilimia 80 kati yao tayari wanatumia mizani iliyokaguliwa na kugongwa muhuri wa Wakala wa Vipimo Tanzania.
Naye mfanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo, Khadija Abdallah, amesema wafanyabiashara wamekuwa wakikumbana na changamoto ya kutokuaminiwa na wateja kutokana na matumizi ya vipimo visivyo rasmi kama makopo na mifuko.
Amesema kupatiwa mizani kutasaidia kurejesha imani ya wateja na kuongeza uwazi katika biashara zao.