Wanufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi yanayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu wakiwa katika mafunzo ya vitendo kwenye Chuo cha Annacollection Fashion Academy (AFA), Jijini Dar es Salaam.
Na: OWM (KAM) – Dar es Salaam
Serikali imeendelea kuweka mikakati mbalimbali ya kuwawezesha vijana nchini ikiwemo utekelezaji wa Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi kupitia Mafunzo ya Uanagenzi imeendelea kuwa mwanga wa matumaini kwa vijana wengi nchini.
Programu hiyo ambayo inatekelezwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano tangu mwaka 2016 imekuwa ni chachu ya kuwezesha nguvu kazi ya Taifa hususan vijana kupata ujuzi na stadi za kazi stahiki zitakazowasaidia vijana kujiajiri na hatimaye kuondokana na changamoto ya ajira. Eneo moja wapo la utekelezaji wa Programu hii ni Mafunzo ya Kukuza Ujuzi kwa vijana kwa njia ya Uanagenzi (Apprenticeship Training) ambayo yamekuwa kichocheo kikubwa cha uwekezaji, biashara na kukuza kipato cha watanzania.
Vijana wengi wameanza kuona mwanga wa maisha kwa kupata ujuzi na mafunzo ya vitendo katika Vyuo vya Ufundi Standi mbalimbali vilivyopo nchini. Miongoni mwa vijana wanaonufaika na mafunzo ni wanafunzi wa Chuo cha Anna Collections Fashion Academy (AFA) ambao wameeleza namna mafunzo hayo yanavyowasaidia kujijengea uwezo wa kujitegemea kiuchumi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Wanagenzi hao akiwemo Jesca Machimu ambaye ni mwanagenzi katika fani ya Ushonaji na Ubunifu wa Mavazi, ameishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano kwa kuwapatia mafunzo ya ujuzi ambayo yanayowawezesha kupata maarifa na ujuzi.
“Nilikuwa ni kijana ambaye nipo tu mtaani, niliposikia Serikali imetangaza fursa hii ya mafunzo ya Unagenzi nilichangamkia na nipo hapa katika Chuo cha Ubunifu wa Mavazi Anna Collection Fashion Academy na hadi sasa ninaweza kushona mavazi ya aina mbalimbali,” amesema
Naye, Asia Selemani Matauna amesema mafunzo hayo ni fursa kubwa kwake kwani yatamjengea uwezo mkubwa katika tasnia ya ubunifu wa mavazi. Amesema ndoto yake ni kufungua kampuni yake binafsi baada ya kuhitimu na kuajiri vijana wengine ili nao waweze kupata kipato na kujitegemea.
Vilevile, Rashidi Mohamed amesema kabla ya kujiunga na mafunzo hayo alikuwa akishonea nyumbani kwa kiwango cha kawaida, lakini kupitia programu ya uanagenzi ameweza kupata maarifa ya kisasa zaidi yatakayomsaidia kupanua biashara yake na kuongeza kipato chake.
Kadhalika, Mratibu wa Mafunzo kutoka Anna Collections Fashion Academy, Bw. Stephen Mliga amesema kuwa mwaka 2025/2026 chuo hicho kimepokea wanafunzi wa uanagenzi kwa mara ya kwanza ambapo Serikali imefadhili vijana 126 kujiunga na mafunzo hayo, licha ya kuwa waliomba nafasi kwa vijana zaidi ya 450.
Bw. Stephen amesema vijana wengi wanaopata mafunzo hayo hujengewa fikra za kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa. Ameeleza kuwa kupitia tasnia ya ubunifu wa mavazi, vijana wanaweza kuanzisha biashara zao binafsi, kufungua kampuni ndogo ndogo na kuajiri vijana wengine.
Aidha, amesema tasnia ya fashion inaendelea kukua kwa kasi duniani na kuwa miongoni mwa sekta zinazozalisha ajira nyingi na kipato kikubwa. Amesema matarajio ya AFA ni kuona vijana wa Kitanzania wanashindana kimataifa katika tasnia hiyo, sambamba na kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuwa na vijana wabunifu na wenye kujitegemea kiuchumi.
Kwa mujibu wa Bw. Stephen, dira ya AFA ni kupambana na umaskini kwa kuwainua vijana kupitia ubunifu na ujuzi wa kazi. Ameongeza kuwa chuo hicho kinatarajia kuwa miongoni mwa vyuo bora vya fashion Afrika Mashariki na kupanua huduma zake hadi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ifikapo mwaka 2026/2027.
Katika kuhakikisha vijana wanapata mafunzo kulingana na viwango vya uwezo wao, Annacollections Fashion Academy (AFA) kimeweka mfumo maalum wa madarasa unaolenga kuwajengea wanafunzi uwezo hatua kwa hatua. Mfumo huo unaanza na darasa la awali la Beginner Class kwa vijana wasiokuwa na ujuzi wowote wa ushonaji.
Baada ya hapo, wanafunzi huendelea katika Advanced Class, darasa linalowajengea uwezo wa ubunifu na uzalishaji wa bidhaa za kisasa. Pia kuna Bridal Master Class inayojikita katika ushonaji wa mavazi ya maharusi kwa viwango vya kitaalamu, sambamba na darasa la ushonaji wa suti pamoja na darasa maalum la urembeshaji wa mavazi.

Wanufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi yanayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu wakiwa katika mafunzo ya vitendo kwenye Chuo cha Annacollection Fashion Academy (AFA), Jijini Dar es Salaam.