*●Yalenga kuchangia trilioni 1.4/- za maduhuli*
*●Makusanyo yafikia Trilioni 1 na Milioni 156*
*●Jumla ya tani 23.8 za dhahabu zakusaywa ndani ya miezi 18*
*●Ni Juhudi za Rais.Dkt.Samia Suluhu Hassan*
*Dodoma*
Bunge la Jamhuru ya Muungano wa Tanzania, limeridhia na kupitisha bajeti ya Wizara ya Madini ya shilingi bilioni 174.9 kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 ili kuiwezesha Wizara ya Madini kufanikisha ukusanyaji wa maduhuli ya shilingi trilioni 1.4.
Akiwasilisha Bungeni makadirio ya Mapato na Matumizi leo Aprili 27, 2026, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema fedha hizo zitawezesha kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Wizara pamoja na taasisi zilizo chini yake, huku zikilenga kuendeleza kasi ya ukuaji wa sekta ya madini kwa kufanya tafiti za jiosayansi nchini.
Akifafanua mgawanyo wa Bajeti hiyo, Waziri Mavunde amesema kiasi cha shilingi bilioni 71.5 sawa na asilimia 40.9 zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo, wakati shilingi bilioni 103.5 sawa na asilimia 59.1 zikiwa ni matumizi ya kawaida. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 27.4 ni mishahara ya watumishi na shilingi bilioni 76.1 ni matumizi mengineyo ya Wizara na taasisi zake.
Kuhusu mwenendo wa Sekta, Waziri Mavunde amefanunua kuwa, mchango wa Sekta ya Madini katika kuchangia katika Pato la Taifa umeendelea kuimarika, ukiongezeka kutoka asilimia 9.1 mwaka 2023 hadi asilimia 10.1 mwaka 2024, na kufikia wastani wa asilimia 11.9 mwaka 2025.
Aidha, Waziri Mavunde ameongeza kuwa ukusanyaji wa maduhuli umeongezeka kwa kiwango kikubwa, kutoka shilingi bilioni 753.2 mwaka 2023/2024 hadi shilingi trilioni 1.07 mwaka 2024/2025. Kwa kipindi cha miezi tisa ya mwaka 2025/2026 (Julai hadi Machi), tayari shilingi trilioni 1.03 sawa na asilimia 114.9 ya lengo lililopangwa.
Katika kuimarisha biashara ya madini, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, idadi ya masoko imeongezeka kutoka 43 hadi 44, huku vituo vya ununuzi vikiongezeka kutoka 114 hadi 118, hatua inayolenga kuongeza uwazi na ushindani wa bei kwa wachimbaji.
Ametaja vipaumbele vya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 kuwa ni kuimarisha mchango wa sekta katika uchumi, kuendeleza mnyororo wa thamani madini muhimu na ya kimkakati, pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika uongezaji thamani.
Vipaumbele vingine ni kuimarisha uendeshaji wa minada na maonesho ya madini ya vito, kuongeza uwekezaji katika tafiti za kina za madini, kurasimisha na kuwaendeleza wachimbaji wadogo, ikiwa pamoja na kuzijengea uwezo taasisi zilizo chini ya Wizara ili kuongeza tija na ufanisi.
Kwa upande wake , Naibu Waziri wa Madini Dkt.Steven Kiruswa amesema kuwa , Wizara ya Madini itaendelea kuimarisha ukaguzi katika migodi midogo na mikubwa ili kuongeza ufanisi katika uzalisha madini.
Akielezea kuhusu mageuzi ya utoaji leseni Dkt.Kiruswa amesema kuwa Wizara ipo mbioni kuweka mifumo ya utoaji leseni kidigitali jambo litakalo rahisisha utoaji leseni bila mgongano wa kimaslahi.