Featured Kimataifa

CHUO CHA UTUMISHI WA UMMA TANZANIA KUBORESHA MAFUNZO NA KUWAFIKIA ZAIDI YA WATUMISHI 40,000 MWAKA 2026/27

Written by Alex Sonna

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 17,2026 bungeni Dodoma.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

Serikali kupitia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imepanga mageuzi makubwa ya mafunzo na uendelezaji wa watumishi wa umma kwa mwaka wa fedha 2026/27, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Hayo yamesemwa leo Aprili 17,2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027.

Amesema kuwa  chuo kimejipanga kuendeleza na kuboresha programu mpya 15 za mafunzo katika maeneo ya uongozi, usimamizi na utawala, kwa lengo la kuwajengea uwezo watumishi wa umma katika utendaji kazi wa kisasa na wenye tija.

 “Jumla ya watumishi 10,000 wanatarajiwa kupatiwa mafunzo ya kujiandaa na mitihani ya Utumishi wa Umma ili kuongeza ufanisi na weledi kazini. Sambamba na hilo, watumishi 20,000 watapatiwa mafunzo ya uongozi, menejimenti na usimamizi wa ofisi, huku watumishi wengine 3,000 wakipata mafunzo hayo kwa njia ya mtandao.”amesema Mhe.Ridhiwani

Aidha, watumishi wapya 10,000 watanufaika na mafunzo ya awali yatakayowajengea uelewa wa mifumo ya Serikali na misingi ya utumishi wa umma, hatua inayolenga kuwaandaa kikamilifu katika majukumu yao ya kazi.

Katika kuendana na maendeleo ya teknolojia, TPSC itaboresha miundombinu ya ujifunzaji wa kidijitali ili kuongeza upatikanaji wa mafunzo kwa gharama nafuu na kwa ufanisi zaidi. Hatua hii inalenga kuwafikia watumishi wengi zaidi bila kuathiri ubora wa mafunzo.

Kwa mafunzo ya muda mrefu, washiriki 13,400 watapatiwa elimu katika fani mbalimbali ikiwemo utunzaji wa kumbukumbu, uhazili, TEHAMA, usimamizi wa fedha za umma, rasilimaliwatu, manunuzi ya umma pamoja na uongozi na utawala bora.

Chuo pia kitatoa ushauri wa kitaalamu kwa taasisi 12 za umma ili kusaidia kubaini changamoto za kiutendaji na kutoa mapendekezo ya maboresho yanayotokana na tafiti. Sambamba na hilo, tafiti tumizi 14 na machapisho 20 yatafanyika ili kuchangia maboresho ya sera na utoaji huduma kwa wananchi.

Katika kukuza majadiliano ya kitaalamu, midahalo mitano ya mtandaoni itaratibiwa kwa kushirikisha watumishi wa umma na sekta binafsi, huku watumishi 40 wa chuo wakipatiwa mafunzo ya muda mrefu katika ngazi mbalimbali za elimu kuimarisha uwezo wa ndani wa taasisi.

Kwa upande wa miundombinu, TPSC imepanga kukamilisha awamu ya kwanza ya ujenzi wa kampasi ya Tanga, itakayojumuisha madarasa yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 2,500 kwa wakati mmoja, kumbi za mikutano na ofisi za watumishi. Aidha, ukarabati wa kampasi ya Tabora utafanyika ili kuhamishia baadhi ya programu za muda mrefu, huku juhudi za kupata eneo la kampasi mpya Mbeya zikiendelea.

Kwa ujumla, mpango huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha utumishi wa umma kupitia mafunzo, tafiti na matumizi ya teknolojia, ili kuhakikisha watumishi wanakuwa na ujuzi, maadili na uwezo unaohitajika katika kutoa huduma bora na zenye tija kwa wananchi.

About the author

Alex Sonna