Featured Kitaifa

RAIS SAMIA:’SERIKALI ITATOA KIPAUMBELE KATIKA SEKTA YA KILIMO’

Written by mzalendoeditor

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali imeweka mkazo mkubwa katika sekta za kilimo, uvuvi na ufugaji kuanzia mwaka wa fedha ujao.

Rais Samia amesema hayo wakati akihutubia wananchi wa mkoa wa Tabora katika uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mkoani humo akisisitiza kuwa sekta hizo zinawagusa wananchi moja kwa moja.

Aidha, Rais Samia amesema kilimo cha maeneo makubwa kitasaidia kuondoa uhaba wa bidhaa mbalimbali kama mafuta ya kula hivyo amemuagiza Waziri wa Kilimo kupunguza bajeti ya matumizi ya manunuzi ya mbolea na kuelekeza fedha hizo kwenye kilimo kikubwa.

Rais Samia ametoa wito kwa watafiti wa mbegu za kilimo kufanya utafiti wa mbegu bora za kisasa ili wakulima wapate mbegu zitakazowapa mavuno mazuri.

Pia, Rais Samia amewaagiza Wakuu wa Mikoa pamoja na Wilaya kuhifadhi chakula kilichopo ili kitoshe kutumika kabla ya kupata mvua zingine za uhakika kwa kuwa mwaka huu mavuno yamekuwa haba kutokana na ukosefu wa mvua. 

 

Hali kadhalika, Rais Samia amesema, ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa mvua ambayo inaathiri kilimo, Serikali inaweka mikakati ya kufanya kilimo cha umwagiliaji ambacho hakitotegemea misimu ya mvua.

Kwa upande mwingine, Rais Samia amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakuu wa Wilaya na Maafisa Tawala nchini kuhakikisha kuwa wanasimamia matumizi ya fedha zinazopelekwa katika Halmashauri zao na kuhakikisha zinafanya kazi zilizokusudiwa katika kutoa huduma za kijamii kwa wananchi. 

About the author

mzalendoeditor