Na Dotto Kwilasa,Dodoma
Serikali imeweka wazi kuwa usafi wa mazingira ni nguzo ya msingi katika kulinda afya za wananchi na kuongeza kasi ya maendeleo ya taifa, ikisisitiza haja ya kuimarishwa kwa mifumo jumuishi ya utoaji huduma ili kufikia jamii zote mijini na vijijini.
Hayo yameelezwa leo July 2,2026 jijini Dodoma katika Kongamano la Kitaifa la Usafi wa Mazingira
lililoambatana na uzinduzi wa Mwongozo wa Mipango Jumuishi ya Usafi wa Mazingira wa mwaka 2025 lenye lengo la kuimarisha na kuunganisha jitihada za wadau katika kuboresha huduma jumuishi za usafi wa mazingira nchini, kwa lengo na Kuimarisha mifumo ya usimamizi wa taka ngumu na majitaka ili kupunguza magonjwa yanayotokana na uchafuzi wa mazingira.
Akizungumza kwenye kongamano hilo ,Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Prof.Paramagamba Kabudi amesema
kongamano hilo litasaidi kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika usafi wa mazingira ikiwa ni pamoja na kusaidia utekelezaji wa sera, sheria na miongozo mipya ya mazingira
Kuharakisha maendeleo ya miji na vijiji iliyo safi, salama na endelevu.
Amesema,Serikali ya awamu ya Sita
inayoongozwa na Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele kikubwa katika kuhakikisha mazingira yanabaki salama na rafiki kwa afya ya binadamu.
“Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha Tanzania inakuwa na miji na vijiji safi, salama na vinavyopendeza, akisisitiza kuwa hilo linaweza kufikiwa endapo wananchi watajenga utamaduni wa usafi na kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira yao,”amesema na kuongeza;.
Tunataka Tanzania yenye miji na vijiji safi. Ni muhimu kuja na mikakati madhubuti itakayowezesha upatikanaji wa huduma jumuishi za usafi wa mazingira ili ziwafikie wananchi wote,” amesema Kabudi.
Ametaja pia mchango wa Rais Samia katika ajenda ya Nishati safi, akisema uongozi wake umeiweka Tanzania kwenye ramani ya mataifa yanayoongoza mabadiliko ya matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira.
“Rais Samia amekuwa kinara wa nishati safi duniani,tunapaswa kuendeleza kasi hii ili kuhakikisha wananchi wote wanatumia nishati salama na rafiki kwa mazingira,” amesisitiza.
Aidha, Kabudi amekemea tabia ya baadhi ya wananchi kutumia mitaro ya maji kama sehemu ya kutupia taka, akionya kuwa tabia hiyo inachangia kuziba mifumo ya maji na kuongeza hatari ya mafuriko na magonjwa.
Amesisitiza kuwa uwekezaji katika usafi wa mazingira ni uwekezaji katika afya ya wananchi, akihimiza ulinzi wa vyanzo vya maji na utekelezaji madhubuti wa sera na sheria za mazingira.
Kwa upande wa huduma za kijamii, ametaja umuhimu wa kuboresha miundombinu ya vyoo katika maeneo ya mikusanyiko kama masoko, sambamba na kuhakikisha upatikanaji wa maji ya kunawa mikono ili kudhibiti magonjwa ya mlipuko.
Changamoto nyingine alizozitaja ni ongezeko la makazi holela na athari za mabadiliko ya tabianchi, akipendekeza kuimarishwa kwa mipango miji na upimaji wa viwanja ili kudhibiti ujenzi usio rasmi.
Kwa upande wake,Kwa upande wake Mkurugenzi wa Fedha wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Stanley Mahembe,aliyemwakilishi Mkurugenzi Mkuu EWURA, Stanley Mahembe,amesema takwimu zinaonyesha kuwa kati ya mamlaka 84 za maji nchini, ni 24 pekee ndizo zina mpango wa kutibu majitaka na tope la kinyesi, hali inayoonyesha bado kuna pengo kubwa la utekelezaji.
Ameongeza kuwa kongamano hilo pia limezindua Mwongozo wa Usimamizi wa Mazingira utakaosaidia kuimarisha ufuatiliaji wa huduma za usafi wa mazingira nchini.
“EWURA itaendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha huduma za utibuji wa majitaka na tope la kinyesi zinaimarishwa ili kulinda afya za wananchi na mazingira,” amesema.
Naye Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Ngosi Mwihava, amesema kupitia bajeti ya shilingi trilioni 1.12 iliyopitishwa kwa ajili ya Wizara ya Maji, kuna matumaini makubwa ya kuimarisha ujenzi wa miundombinu ya maji taka na usafi wa mazingira, ili kuendana na lengo la Maendeleo Endelevu (SDG) namba 6 linalohusu upatikanaji wa maji safi na usafi wa mazingira kwa wote.
Kwa upande wake Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira Bunge la Tanzania Kunti Majala aliipongeza EWURA kwa kuandaa kongamano hilo, akisema limeweka msingi wa maboresho ya usimamizi wa sekta ya mazingira nchini.
Amesema vifo vinavyotokana na athari za mazingira mara nyingi husababishwa na shughuli za binadamu, hivyo elimu kwa wananchi inapaswa kupewa kipaumbele ili kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika, hususan kwa watoto.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri, amesema kasi ya ongezeko la watu katika mkoa huo imeongeza uhitaji wa mifumo imara ya usafi wa mazingira, akisisitiza kuwa wilaya ipo tayari kutekeleza miongozo mipya itakayowekwa ili kuboresha hali ya mazingira.
