Kampuni ya usafiri wa mtandao ya Bolt Tanzania jana iliwapokea wanafunzi kutoka programu ya Oasis Summer Camp 2026 katika Kituo cha Huduma kwa Madereva (Driver Engagement Centre – DEC) jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya ziara ya mafunzo iliyolenga kuwajengea uelewa kuhusu teknolojia, ubunifu na usalama katika matumizi ya huduma za usafiri wa kidijitali.
Ziara hiyo, iliyoandaliwa kwa ushirikiano na Oasis Village Club, iliwapa wanafunzi wa shule za msingi fursa ya kujionea kwa karibu namna makampuni ya kidijitali yanavyobadilisha huduma za usafiri na kuimarisha viwango vya usalama kwa madereva na abiria.
Katika mafunzo hayo, wanafunzi walitambulishwa baadhi ya zana za usalama zinazotumiwa na Bolt, ikiwemo mfumo wa kushirikisha taarifa za safari (Trip Sharing), ufuatiliaji wa safari kwa wakati halisi (Ride Tracking), huduma ya msaada wa dharura, uthibitishaji wa madereva pamoja na mifumo ya huduma kwa wateja inayoongeza uwajibikaji na uwazi katika kila safari.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Meneja wa Nchi wa Mawasiliano ya Bolt Tanzania, Gilbert Ginono, alisema kampuni inaamini kuwa kuwawezesha vijana kupitia elimu ni uwekezaji muhimu kwa mustakabali wa taifa.
“Tunaamini elimu ni miongoni mwa nyenzo muhimu zinazowawezesha vijana kuelewa namna teknolojia inavyoweza kubadilisha simulizi la changamoto zinazozikabili jamii zetu. Kupitia ziara kama hizi, wanafunzi hupata fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu ubunifu wa Bolt unaowezesha madereva na abiria kusafiri kwa usalama.
Tunatarajia kuendeleza ushirikiano na shule pamoja na vyuo vikuu ili kuwaonesha namna teknolojia ilivyoboresha usalama wa usafiri leo ukilinganisha na miaka kumi iliyopita, ambapo kusafiri usiku kulikuwa na hofu kubwa zaidi na abiria hawakuwa na njia rahisi za kuthibitisha madereva au kushirikisha taarifa za safari zao na wapendwa wao.”
Programu ya Oasis Summer Camp imeendelea kujizengea sifa kwa kuwapatia wanafunzi kutoka shule mbalimbali za Dar es Salaam fursa ya kutembelea taasisi na sekta tofauti, hatua inayowawezesha kupata maarifa na uzoefu wa vitendo nje ya mazingira ya darasani.
Bolt Tanzania imesisitiza kuwa itaendelea kuunga mkono mipango inayokuza matumizi salama ya teknolojia, uelewa wa masuala ya usalama pamoja na ubunifu kwa wanafunzi wa shule na vyuo vikuu, ikiwa ni sehemu ya kuandaa kizazi kijacho kwa uchumi wa kidijitali.
