Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma
Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kulipa madeni ya wakandarasi, wazabuni na watumishi ili kuimarisha mazingira ya biashara, kuongeza ushiriki wa wazawa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kulinda mitaji ya vijana wanaojihusisha na shughuli mbalimbali za kiuchumi nchini.
Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Timida Mpoki Fyandomo, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kulipa madeni ya wakandarasi na wazabuni.
Mhe. Luswetula alisema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imekuwa ikitenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kugharamia ulipaji wa madeni hayo ili kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo unaendelea kwa ufanisi na sekta binafsi inaendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
“Katika mwaka wa fedha 2025/26, Serikali ilitenga shilingi bilioni 700 kwa ajili ya kulipa madeni ya wakandarasi, wazabuni na watumishi ambapo hadi Februari 2026 jumla ya shilingi bilioni 477.6 zilikuwa tayari zimetolewa,” alisema Mhe. Luswetula.
Aliongeza kuwa Serikali imetenga shilingi bilioni 800 katika mwaka wa fedha 2026/27 kwa ajili ya kugharamia ulipaji wa madeni yaliyohakikiwa, hatua itakayosaidia kuimarisha uwezo wa wakandarasi na wazabuni wa ndani kushiriki katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Aidha, alisema Serikali imeendelea kutoa maelekezo kwa Maafisa Masuuli kuhakikisha bajeti za kulipa madeni zinatengewa fedha, matumizi yanadhibitiwa kupitia mifumo rasmi ya Serikali na michakato ya manunuzi inaanzishwa pale tu ambapo kuna uhakika wa upatikanaji wa fedha.
Mhe. Luswetula alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kulipa madeni yaliyohakikiwa kwa wakati ili kuimarisha mazingira ya biashara, kuongeza imani kwa wawekezaji wa ndani na kuwezesha wananchi, hususan vijana, kunufaika zaidi na fursa zinazotokana na miradi ya maendeleo inayotekelezwa nchini.