Chamwino, Dodoma
Wananchi wa wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma wameendelea kunufaika na maboresho ya miundombinu yanayotekelezwa na Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) huku Daraja la Mlowa Barabarani likitajwa kuwa miongoni mwa miradi iliyorejesha matumaini na kurahisisha maisha ya wananchi katika eneo hilo.
Daraja hilo lenye urefu wa mita 32 lililojengwa katika barabara ya Mlowa Barabarani–Ngheherezi yenye urefu wa kilomita 32 limekuwa suluhisho la changamoto ya muda mrefu iliyokuwa ikiwasumbua wananchi hususan nyakati za mvua.
Akizungumza kuhusu utekelezaji wa miradi hiyo, Meneja wa TARURA wilaya ya Chamwino Mhandisi Richard Sanga alisema, TARURA wilayani humo inahudumia mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 1,397 na imeendelea kufanya matengenezo ya barabara pamoja na ujenzi wa madaraja ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za usafiri na usafirishaji.
Alisema kabla ya ujenzi wa daraja hilo wananchi walikuwa wakikumbwa na adha kubwa ya kuvuka mto huo hali iliyosababisha ugumu wa kufikia huduma muhimu za kijamii na kiuchumi ikiwemo shule, hospitali na masoko.
”Daraja hili limekuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi hapo awali mvua zikinyesha wananchi walikuwa wakishindwa kuvuka mto na kushindwa kufika kwenye huduma muhimu za kijamii lakini sasa usafiri ni rahisi na shughuli za maendeleo zinaendelea vizuri”, alisema Mhandisi Sanga.
Aidha, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya miundombinu inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.
Daraja hilo linaunganisha kata za Mlowa Barabarani, Makang’wa, Iringa Mvumi na Ngheherezi hatua ambayo imeongeza mzunguko wa shughuli za kiuchumi katika maeneo hayo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mlowa B, Bw. Moses Chilamba alisema kabla ya daraja kujengwa
wakati wa mvua mto ukijaa ulikuwa unatenganisha kijiji cha Mlowa B na kitongoji cha Magaga ambako kuna shule ya msingi. Pia wakulima walikuwa wanashindwa kusafirisha mazao yao kwenda sokoni lakini sasa daraja hilo limekuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi.
Naye, mkazi wa kijiji cha Mlowa Barabarani Bi. Stella Chelula alisema, kipindi cha mvua wanawake wajawazito walishindwa kuvuka mto wakati mwingine akina mama walikuwa wanajifungulia njiani kwa kushindwa kwenda kituo cha afya lakini sasa magari na pikipiki zinapita kwa urahisi na usafiri umeimarika.
Ujenzi wa Daraja la Mlowa Barabarani ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita za kuboresha miundombinu vijijini na mijini kupitia TARURA hatua inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.
