Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe,akizungumza wakati akifungua mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu na usafi wa miji leo Mei 12,2026 jijini Dodoma,

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule,akizungumza wakati wa mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu na usafi wa miji leo Mei 12,2026 jijini Dodoma,

Mkurugenzi Msaidizi wa Mabadiliko ya Tabianchi na Tathmini kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Dk Kanizio Manyika,akizungumza wakati wa mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu na usafi wa miji leo Mei 12,2026 jijini Dodoma,

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe (hayupo pichani) wakati akifungua mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu na usafi wa miji leo Mei 12,2026 jijini Dodoma,
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuimarisha usimamizi wa taka ngumu na usafi wa mazingira nchini, huku ikizitaka halmashauri zote kurejesha asilimia 10 ya mapato yatokanayo na shughuli za udhibiti wa taka kwa ajili ya kuimarisha huduma za usafi wa mazingira.
Akifungua mkutano wa mwaka wa tathmini ya utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu na usafi wa miji jijini Dodoma, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imejipanga kuhakikisha miji na maeneo ya makazi yanakuwa safi, salama na yenye mazingira bora kwa wananchi.
Prof. Shemdoe amesema kuongezeka kwa ufanisi katika ukusanyaji na usimamizi wa taka kutasaidia vitengo vya usafi wa mazingira kupata fedha zaidi za kuendesha shughuli zao kwa ufanisi.
“Kadri mtakavyoongeza ufanisi katika udhibiti wa taka, ndivyo vitengo vyenu vitakavyopata fedha zaidi kwa ajili ya kutekeleza kazi hii muhimu,” amesema Prof. Shemdoe
Aidha, amesema serikali inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo, ikiwemo Japan, kutafuta teknolojia za kisasa za uteketezaji na urejelezaji wa taka ngumu ili kupata suluhisho la kudumu la changamoto hiyo.
Amebainisha kuwa tayari maandalizi ya majaribio ya matumizi ya teknolojia hizo yanafanyika katika baadhi ya miji nchini, hatua inayotarajiwa kuleta mapinduzi katika sekta ya usimamizi wa taka.
Katika hatua nyingine, Prof.Shemdoe amezielekeza halmashauri zote nchini kuanzisha maeneo rasmi ya kutupia taka ili kudhibiti uchafuzi wa mazingira na kupunguza hatari ya milipuko ya magonjwa.
“Bado baadhi ya halmashauri hazina maeneo rasmi ya kutupia taka, hali inayodhoofisha juhudi za usafi na uhifadhi wa mazingira,” amesema
Pia amewahamasisha vijana na wanawake kutumia mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kuanzisha shughuli za ukusanyaji, uchakataji na urejelezaji wa taka, akisema taka zinaweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira na mapato.
“Taka kama chupa za plastiki zinaweza kuuzwa kwa kampuni za urejelezaji na kusaidia wananchi kujiongezea kipato huku wakichangia usafi wa mazingira,” amesema
Prof. Shemdoe alieleza kuwa kuimarika kwa usafi wa mazingira tayari kumechangia kupungua kwa magonjwa ya mlipuko ikiwemo kipindupindu katika baadhi ya maeneo nchini.
“Tunapoongeza usafi tunapunguza matumizi makubwa ya fedha za matibabu na fedha hizo zinaweza kuelekezwa kwenye miradi mingine ya maendeleo,” amesisitiza.
Aidha, ametaka suala la usafi wa mazingira kuwa ajenda ya kudumu katika vikao vya maamuzi kuanzia ngazi ya mkoa hadi vijiji na mitaa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema mkoa huo umeongeza bajeti ya usafi wa mazingira kutoka Sh milioni 750 hadi Sh bilioni 3 kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Amesema fedha hizo zitatumika kununua vifaa vya usafi, kuimarisha ukusanyaji wa taka pamoja na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira.
Naye Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia afya katika Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Profesa Tumaini Nagu, amesema serikali itaendelea kuviimarisha vitengo vya usafi wa mazingira ili kuongeza ufanisi wa huduma hizo katika miji mbalimbali nchini.
Mkurugenzi Msaidizi wa Mabadiliko ya Tabianchi na Tathmini kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Dk Kanizio Manyika, amesema Tanzania huzalisha zaidi ya tani milioni 17 za taka ngumu kila mwaka, huku asilimia 60 hadi 75 ya taka hizo zikibaki kwenye mazingira kutokana na kutokusanywa ipasavyo.
Naye Mwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Joseph Birango, amesema takwimu zinaonesha magonjwa sita kati ya 10 yanayoikumba jamii yanachangiwa na uchafuzi wa mazingira na ukosefu wa mifumo bora ya usimamizi wa taka.
“Hivyo kuna haja ya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu usafi wa mazingira ili kupunguza magonjwa ya mlipuko pamoja na gharama za matibabu,” amesema
Awali, Mwenyekiti wa Wakuu wa Vitengo vya Udhibiti wa Taka na Usafi wa Mazingira Tanzania Bara, William Mpangala kutoka Wilaya ya Bahi, anmeiomba serikali kutoa maelekezo madhubuti yatakayohakikisha asilimia 10 ya mapato yatokanayo na udhibiti wa taka yanarejeshwa kwenye shughuli za usafi wa mazingira.