#Barabara zafunguliwa kusaidia wakulima kufikia masoko
Njombe
Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) mkoa wa Njombe imeendelea kuimarisha miundombinu ya barabara kwa kasi, hatua inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa mkoa huo.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa wananchi mkoani wa Njombe, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali Ndugu Gerson Msigwa alisema, TARURA mkoa wa Njombe inasimamia mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 5,208.04 ambapo kati ya hizo kilomita 95.51 ni za lami, kilomita 2,097.40 ni changarawe na kilomita 3,015.13 ni barabara za udongo.
Alisema asilimia 70.96 sawa na kilomita 3,688.59 za mtandao huo ziko katika hali nzuri na zinapitika majira yote ya mwaka, huku asilimia 29.04 sawa na kilomita 1,519.45 zikipitika kwa changamoto zaidi wakati wa mvua.
Kwa mujibu wa Msigwa, vipaumbele vya TARURA Njombe ni pamoja na matengenezo ya barabara zilizopo, ujenzi wa miundombinu ya kuvuka mito ikiwemo madaraja na “concrete strips”, kufungua barabara mpya ili kufikia kata na vijiji ambavyo hapo awali havikufikika kwa urahisi pamoja na kuboresha barabara za lami na changarawe.
“Tunafungua pia barabara mpya katika maeneo ya uzalishaji wa mazao ya kimkakati kama parachichi, chai, viazi na ngano ili kuongeza tija kwa wakulima na kukuza uchumi wa wananchi na hivyo kuweza kuyafikia masoko,” alisema Msigwa.
Katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, bajeti ya TARURA mkoa wa Njombe imeongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 8.44 kwa mwaka kati ya 2017 hadi 2021 na kufikia bilioni 21.07 kwa mwaka kati ya 2021 hadi 2026, sawa na ongezeko la asilimia 149.64.
Ongezeko hilo limewezesha mafanikio makubwa katika sekta ya barabara ambapo urefu wa barabara za lami umeongezeka kutoka kilomita 38.71 mwaka 2020 hadi kilomita 95.51 mwaka 2026. Vilevile, barabara za changarawe zimeongezeka kutoka kilomita 1,255.62 hadi kilomita 2,097.40 huku barabara za udongo zikipungua kutoka kilomita 3,913.71 hadi kilomita 3,015.13.
Kwa upande wa miundombinu ya madaraja na vivuko, idadi ya madaraja imeongezeka kutoka 352 hadi 386, kalavati kutoka 2,535 hadi 2,962 na taa za barabarani kutoka 27 hadi 365.
Miradi mingine iliyotekelezwa ni pamoja na ufunguaji wa barabara katika mwambao wa Ziwa Nyasa wilayani Ludewa, kuunganisha maeneo ya Igagala-Lugenge (Usalule-Nole), Utengule-Wanging’ombe pamoja na ujenzi wa barabara za lami Njombe Mjini zenye kilomita 5.1 na Ukomola-Ipwani kilomita 6.7 ambapo zaidi ya kilomita 46 za barabara mpya zimefunguliwa katika mkoa mzima.
Utekelezaji wa miradi hiyo umechangia utoaji wa ajira kwa vijana na wanawake, kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya, elimu, masoko na viwanda pamoja na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Msigwa ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Njombe kuendelea kutunza miundombinu iliyojengwa ili idumu na kuwanufaisha kizazi cha sasa na kijacho.
“Serikali chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuongeza nguvu na bajeti kwa TARURA ili kuhakikisha barabara zinapitika mwaka mzima, kuwawezesha wakulima na kuimarisha uchumi wa Taifa,” alisema.
