Na Atley Kuni, WAF – Dodoma
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI imeishauri Serikali kutenga zaidi ya shilingi bilioni 300 kwa ajili ya kuiwezesha Bohari ya Dawa (MSD), hatua inayolenga kuhakikisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba unaendelea kuwa wa uhakika kwa hospitali na vituo vya afya nchini.
Ushauri huo umetolewa bungeni na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dkt. Zeyana Abdallah Mei 11, 2026 jijini Dodoma wakati akiwasilisha maoni ya Kamati kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Dkt. Zeyana ameitaka Serikali kuongeza uwekezaji katika mifumo ya kinga pamoja na kuzijengea uwezo taasisi zake ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za afya, hatua inayokwenda sambamba na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Ilani ya CCM 2025–2030 na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya mwaka 2030.
Katika eneo la rasilimali watu, Kamati imeishauri Serikali kuendelea kutoa vibali vya ajira kwa kada zenye upungufu mkubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya, huku ikisisitiza ajira hizo zitolewe kwa kuzingatia mahitaji halisi ya taasisi pamoja na kuwapa kipaumbele wataalam wanaojitolea katika hospitali mbalimbali nchini.
“Tunaitaka Serikali kuongeza ufadhili wa masomo kwa wataalam wa afya ili kupata mafunzo ya ubingwa na ubingwa bobezi ndani na nje ya nchi, hatua itakayo ongeza wataalam wenye ujuzi wa hali ya juu katika sekta ya afya” amesema Dkt. Zeyana.
Pamoja na ushauri huo, Kamati imeipongeza Serikali kwa maboresho makubwa yanayoendelea kufanyika kwenye sekta ya afya ikiwemo kuanza kwa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, kuimarisha Hospitali za Rufaa za Mikoa na Kanda pamoja na mpango wa ujenzi wa Hospitali mpya ya Taifa ya Muhimbili.
Makamu mwenyekiti huyo ameonesha kuridhishwa na hatua ya Serikali kuendelea kununua vifaa tiba vya kisasa kama mashine za PET CT Scan, MRI, Angio Suite na Mammography, hatua inayochangia kupunguza rufaa za wagonjwa kwenda nje ya nchi na kuokoa fedha za kigeni.
Akihitimisha maoni hayo, Dkt. Zeyana amesema hakuna maendeleo ya kweli yanayoweza kupatikana bila uwekezaji madhubuti katika sekta ya afya, akisisitiza kuwa afya bora ya wananchi ndiyo msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.