Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 7,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imepanga kuchapisha na kusambaza jumla ya nakala milioni nane za vitabu vya kiada pamoja na miongozo ya walimu katika shule za msingi na sekondari nchini kwa lengo la kuboresha ubora wa ufundishaji na kuhakikisha kila mwanafunzi anapata kitabu chake.
Hayo yameelezwa leo bungeni na Waziri wa Wizara hiyo,Prof Adolf Mkenda wakati akiwasilisha mapato na matumizi ya Wizara hiyo Kwa mwaka wa fedha 2026-2027.
Mpango huo unatekelezwa katika mwaka wa fedha 2026/27 na unalenga kuimarisha uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja (1:1), hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi wa ujifunzaji na kuboresha matokeo ya kitaaluma kwa wanafunzi wa ngazi mbalimbali.
Amesema kuwa kati ya nakala hizo milioni 8, jumla ya nakala 3,102,263 zitasambazwa kwa shule za msingi darasa la sita, huku nakala 4,558,899 zikitolewa kwa wanafunzi wa kidato cha tatu katika mkondo wa jumla. Aidha, nakala 338,838 zitatumika kwa wanafunzi wa kidato cha nne katika mkondo wa elimu ya amali.
Katika hatua nyingine, Serikali imeeleza kuwa itaandaa na kusambaza jumla ya nakala 51,000 za vitabu vya kiada vilivyo katika maandishi yaliyokuzwa na mfumo wa Breli kwa ajili ya wanafunzi wenye uoni hafifu na wasioona. Kati ya hizo, nakala 23,000 zitatolewa kwa shule za msingi darasa la sita, nakala 2,000 kwa wanafunzi wa sekondari kidato cha nne mkondo wa amali na nakala 26,000 kwa kidato cha tatu mkondo wa jumla.
Hatua hiyo inalenga kuhakikisha usawa katika upatikanaji wa elimu kwa watoto wote bila kujali changamoto zao za kiafya, sambamba na kuimarisha ujumuishi katika mfumo wa elimu nchini.
Serikali imesisitiza kuwa mpango huo ni sehemu ya jitihada zake za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, kuongeza ubora wa elimu na kuhakikisha kila mwanafunzi anapata rasilimali muhimu za kujifunzia kwa wakati.