Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 7,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeendelea na maandalizi ya utekelezaji wa mpango wa elimu ya lazima ya miaka 10 unaotarajiwa kuanza rasmi Januari 2028, ambapo zaidi ya wanafunzi milioni 3 wanategemewa kuingia katika mfumo huo mpya wa elimu nchini.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda wakati akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Hatua hiyo ni sehemu ya mageuzi makubwa ya sekta ya elimu yanayolenga kuhakikisha kila mtoto wa Kitanzania anapata fursa ya kusoma kwa muda wa kutosha hadi kufikia kiwango cha kuwa tayari kuingia katika soko la ajira au kujiajiri mwenyewe.
Amesema kuwa mpango huo utahusisha wanafunzi wa darasa la sita na la saba kuanza masomo kwa pamoja katika mfumo ulioboreshwa wa elimu ya msingi na sekondari. Ingawa utekelezaji wake unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia itashirikiana kwa karibu katika maandalizi muhimu ikiwemo uandaaji wa miongozo, ujenzi wa miundombinu ya shule, ununuzi wa vifaa vya kujifunzia pamoja na mafunzo kwa walimu.
Serikali imeeleza kuwa tayari imeanza kupanga mikakati ya kuhakikisha miundombinu ya elimu inakidhi mahitaji ya ongezeko la wanafunzi litakalotokana na mfumo huo mpya. Hii ni pamoja na kuongeza madarasa, mabweni, vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na kuimarisha rasilimali watu katika sekta ya elimu.
Katika hatua nyingine, Serikali inaendelea kukamilisha mapitio ya Sheria ya Elimu, Sura ya 353 pamoja na sheria za taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Taasisi hizo ni pamoja na Taasisi ya Elimu Tanzania, Mamlaka ya Elimu Tanzania, Baraza la Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Baraza la Mitihani la Tanzania na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu. Lengo ni kuhakikisha mfumo wa elimu unakuwa imara na unaendana na mabadiliko ya kisera na kimataifa.
Vilevile, Serikali itakamilisha mapitio ya Sera ya Sayansi na Teknolojia ya mwaka 1996 ili kuendana na mahitaji ya sasa ya maendeleo ya kisayansi, teknolojia na ubunifu. Hatua hiyo inalenga kuweka mfumo madhubuti wa kitaifa wa kusimamia sekta ya sayansi na teknolojia kwa kuzingatia vipaumbele vya maendeleo ya nchi.
Kwa ujumla, mipango hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha sekta ya elimu na sayansi kama nguzo kuu ya maendeleo ya taifa, ikiwa na lengo la kujenga kizazi chenye ujuzi, maarifa na uwezo wa kushindana katika uchumi wa kisasa.