Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 30,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMAA
Serikali kupitia Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari imeweka bayana vipaumbele nane vitakavyoongoza utekelezaji wa majukumu yake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, hatua inayotarajiwa kuimarisha kasi ya mageuzi ya kidijitali na kukuza uchumi wa kisasa nchini.
Hayo yamesemwa leo Aprili 30, 2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Waziri Kairuki amesema kuwa wizara inalenga kuboresha mazingira ya sekta ya TEHAMA ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia duniani.
Miongoni mwa vipaumbele vilivyotajwa ni pamoja na kutunga na kuhuisha sera na miongozo ya sekta, kuimarisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano ya simu na posta, pamoja na kuweka mazingira rafiki ya kukuza biashara mtandao. Aidha, serikali inalenga kuendeleza miundombinu ya TEHAMA na kuhakikisha nchi inanufaika kikamilifu na uchumi wa kidijitali.
“Wizara imejipanga kuimarisha ulinzi wa anga ya mtandao ili kukabiliana na vitisho vya kidijitali vinavyoendelea kuongezeka, sambamba na kuchochea ubunifu kwa kusaidia kampuni changa (startups) kupata mazingira bora ya kukua.”amesema Waziri Kairuki
Amesema uwekezaji katika TEHAMA na programu za anga za juu pia umepewa kipaumbele, huku elimu kwa umma kuhusu matumizi sahihi ya teknolojia na teknolojia zinazoibukia ikipewa uzito wa kipekee.
Katika utekelezaji wa majukumu yake, wizara imepanga kuendeleza sera muhimu ikiwemo Sera ya Anga za Juu ya mwaka 2026 na kukamilisha Sheria ya Anwani za Makazi, hatua itakayorahisisha utambuzi wa maeneo na utoaji wa huduma kwa wananchi.
Sekta ya mawasiliano inatarajiwa kushuhudia maboresho makubwa kupitia miradi ya kupeleka huduma za simu na redio katika maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara, pamoja na kupanua huduma za posta nchini. Vilevile, serikali itaendelea kuratibu mradi wa kurusha satelaiti ndogo ya mafunzo (CUBESAT), ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uwezo wa kitaifa katika teknolojia za anga.
Katika eneo la miundombinu, wizara itasimamia ufanisi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano na vituo vya kuhifadhi data, huku ikitekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Brodibendi na Mpango Kabambe wa Miundombinu ya TEHAMA wa mwaka 2026–2036.
Aidha, katika kukuza huduma za kidijitali, serikali imepanga kuanzisha Mpango wa Kitaifa wa Mageuzi ya Kidijitali, kuratibu uanzishwaji wa vituo saba vya ubunifu, na kuwezesha uuzaji wa mifumo ya TEHAMA nje ya nchi.
Hatua hizi zinatarajiwa kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ubunifu na teknolojia katika ukanda wa Afrika Mashariki, huku zikichochea ajira, ubunifu na ushindani wa kiuchumi katika enzi ya kidijitali.