Featured Kitaifa

UDOM YANUFAIKA NA MDAHALO WA ELIMU YA SHERIA NA MATUMIZI SAHIHI YA TEHAMA

Written by Alex Sonna

Mkurugenzi wa Huduma za Msaada wa Sheria, Esther Msambazi,akizungumza wakati wa mdahalo na wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) uliofanyika jijini Dodoma  katika mwendelezo wa kampeni ya Mama Samia Legal Aid, awamu ya pili.

Mkurugenzi wa TEHAMA kutoka Mahakama ya Tanzania, Bw. Kalege Enock,akizungumza wakati wa mdahalo na wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) uliofanyika jijini Dodoma  katika mwendelezo wa kampeni ya Mama Samia Legal Aid, awamu ya pili.

 Amidi wa Shule Kuu ya Sheria Chuo Kikuu cha Dodoma, Dkt. Elia Mwanga,akizungumza wakati wa mdahalo na wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) uliofanyika jijini Dodoma  katika mwendelezo wa kampeni ya Mama Samia Legal Aid, awamu ya pili.

Sehemu ya washiriki wakifuatilia mada mbalimbali  wakati wa mdahalo na wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) uliofanyika jijini Dodoma  katika mwendelezo wa kampeni ya Mama Samia Legal Aid, awamu ya pili.

Mkurugenzi wa Huduma za Msaada wa Sheria, Esther Msambazi,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya  mdahalo na wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) uliofanyika jijini Dodoma  katika mwendelezo wa kampeni ya Mama Samia Legal Aid, awamu ya pili.

Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA

Wizara ya Katiba na Sheria imesema matumizi sahihi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yana mchango mkubwa katika kusogeza huduma za msaada wa kisheria karibu zaidi na wananchi, hasa vijana, kwa urahisi na kwa wakati.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Msaada wa Sheria, Esther Msambazi, wakati wa mdahalo na wanachuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) uliofanyika jijini Dodoma  katika mwendelezo wa kampeni ya Mama Samia Legal Aid, awamu ya pili.
Akizungumza na wanachuo hao, Msambazi amesema  kuwa uwekezaji katika elimu ya kisheria kwa vijana ni hatua muhimu ya kujenga jamii inayotambua haki na wajibu wake. Ameeleza kuwa mdahalo huo unalenga kuwawezesha vijana kuelewa masuala ya kisheria, kujitambua, na kujua wapi pa kupata msaada wanapokumbana na changamoto.
“Vijana wakipata maarifa sahihi ya sheria, wanakuwa si tu walinzi wa haki zao, bali pia wanakuwa nguzo ya kuelimisha jamii,” amesema Bi.Msambazi
Amefafanua kuwa Wizara inaendelea kutumia mbinu za kisasa, hususan TEHAMA, ili kupanua wigo wa huduma za msaada wa kisheria na kuhakikisha zinawafikia wananchi wengi zaidi bila vikwazo vya kijiografia.
Katika mdahalo huo, mada mbalimbali zilijadiliwa ikiwemo ukatili wa kijinsia, matumizi ya mitandao ya kijamii kwa manufaa ya kijamii, pamoja na madhara yanayotokana na matumizi mabaya ya teknolojia.
Hata hivyo Msambazi amesisitiza kuwa TEHAMA imekuwa nyenzo muhimu kwa vijana kupata taarifa sahihi, kuwasiliana na wataalamu wa sheria, na hata kupata msaada bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa TEHAMA kutoka Mahakama ya Tanzania, Bw. Kalege Enock, amesema  ushiriki wa vijana katika masuala ya kisheria ni msingi wa kujenga taifa lenye haki, amani na mshikamano.
Ameongeza kuwa kampeni ya Mama Samia Legal Aid inalenga kuibua kizazi chenye uelewa mpana wa sheria na kinachoweza kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.
Akigusia suala la migogoro, Enock amehimiza matumizi ya njia mbadala za utatuzi, akisema zinaokoa muda, gharama na kusaidia kudumisha mahusiano mema katika jamii.
“Si kila mgogoro unahitaji kufika mahakamani. Zipo njia rafiki zinazoweza kumaliza matatizo kwa haraka na kwa maelewano,” ameeleza.
Naye Amidi wa Shule Kuu ya Sheria UDOM, Dkt. Elia Mwanga, amesema mdahalo huo umefungua upeo wa wanafunzi na kuwapa hamasa ya kushiriki katika utoaji wa msaada wa kisheria.
Amesisitiza kuwa wanafunzi hao wana nafasi ya kipekee ya kuwa mabalozi wa mabadiliko, wakisambaza elimu ya sheria katika maeneo wanayotoka.
“Kwa kuwa chuo hiki kina wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, watakuwa mabalozi wazuri wa kusambaza elimu ya kisheria na kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo kwa urahisi,” amesema Dkt. Mwanga.
Baadhi ya wanachuo walioshiriki wameeleza kufurahishwa na mdahalo huo, wakisema umewapa ujasiri na maarifa ya kutetea haki zao kwa njia sahihi.
Kwa ujumla, mdahalo huo umeonesha wazi kuwa vijana wana nafasi kubwa katika kuimarisha upatikanaji wa haki, ikiwa watapewa elimu sahihi na kushirikishwa kikamilifu katika mifumo ya kisheria.

About the author

Alex Sonna